NA CHARLES WASONGA
IMEBAINIKA kuwa usimamizi mbaya wa mchujo wa ODM kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022 ni mojawapo sababu kuu zinazochangia uasi unaoshuhudiwa katika chama hicho.
Duru zimeiambia safu hii kwamba baadhi ya wabunge ambao wameamua kumkaidi kiongozi wa chama hicho na kuunga mkono serikali ya Rais William Ruto wanafanya hivyo kutokana na “hasira ya kuhangaishwa wakati wa mchujo wa chama hicho”.
“Hawa ambao walienda Ikulu na wengine ambao wameamua kwenda kinyume na msimamo wa Jakom (Raila) wanafanya hivyo kutokana na hasira zinazotokana na kuhangaishwa kwao wakati wa mchujo wa ODM. Wao ni wabunge kama vile Mbunge wa Gem Elisha Odhiambo, Gideon Ochanda (Bondo) na Caroli Omondi (Suba Kusini),” anasema afisa mmoja wa ODM ambaye aliomba tulibane jina lake.
Tulipomfikia kwa njia ya simu, Bw Odhiambo alikubali nusra akose nafasi ya kutetea kiti chake cha ubunge kutokana na usimamizi mbaya wa kura za mchujo “lakini sasa hilo ni suala ambalo limepita na ninawashukuru wakazi wa Gem kusimama nami licha ya jaribio la kunipokonya nafasi ya kuwatumikia. kwa muhula wa pili”.
Itakumbukwa kwamba mnamo Aprili 2022, Kamati Kuu ya chama cha ODM kilifutilia mbali ushindi wa Bw Odhiambo katika kura ya mchujo dhidi ya aliyekuwa mshindani wake wa karibu, Jalang’o Midiwo. Kamati hiyo ilidai Bw Odhiambo alichochea fujo wakati wa zoezi hilo, madai ambayo mbunge huyo alipinga vikali.
Dkt Midiwo ni binamuye Bw Odinga na kakake aliyekuwa mbunge wa Gem marehemu Jakoyo Midiwo.
Lakini hatimaye uongozi wa ODM ulilazimika kumkabidhi Bw Odhiambo cheti cha kuwania ubunge baada ya Jopo la Kutatua Mizozo ya Vyama (PPDT) na Mahakama Kuu kuamua kwamba ushindi wa Bw Odhiambo ulikuwa halali.
Taswira sawa na hiyo ilitokea wakati wa mchujo katika eneo bunge la Bondo ambapo chama cha ODM kilijizatiti kumzuia Bw Ochanda kupeperusha bendera yake katika kinyang’anyiro cha ubunge.
Licha ya kushinda katika kura ya mchujo chama kilimkabidhi tiketi ya uteuzi aliyekuwa mpinzani mbunge wa mbunge huyo John Andiwo, hali iliyomfanya Bw Ochanda kuwasilisha kesi katika jopo la PPDT.
Jopo hilo ndilo lilimuokoa mbunge na kuamuru Bodi ya Kitaifa ya Uchaguzi (NEB) imemkabidhi mbunge huyo tiketi ya uteuzi ndipo akaweza kutetetea kiti hicho na kufaulu kurejea bunge.
Uaminifu wa Mbunge Maalum John Mbadi katika ODM pia umetiliwa shaka wiki hii alipotangaza kwamba yuko tayari kujiuzulu wadhifa wake kama mwenyekiti wa kitaifa.
Mbunge huyo, ambaye amekuwa na uhusiano mbaya na baadhi ya wanachama wa ODM tangu kukamilika kwa uchaguzi mkuu uliopita, anasema ametoa mchango wake kwa chama hicho kama mwenyekiti kwa miaka tisa na sasa wakati umetimia kwake kumpisha mtu mwingine.
Katika siku za hivi karibuni, Bw Mbadi ambaye ni mbunge wa zamani wa Suba Kusini, ameelekezewa mishale ya lawama kwa kufeli kuhudhuria mikutano ya hadhara inayoongozwa na Bw Odinga maeneo mbalimbali nchini.
Akiongea na safu hii juzi, Bw Mbadi alisema anamtambua Dkt Ruto kama Rais wa Kenya huku akitoa wito kwa wafuasi wa Azimio kufanyakazi na serikali yake bila kuhamia mrengo wa Kenya Kwanza.
“Nawaomba watu wetu wa Azimio waachane na huu mjadala eti fulani alipata kura fulani. Tusonge mbele ili tuweze kuvuna maendeleo kwa manufaa yetu sote,” anasema huku akipuuzilia mbali ripoti ya mfichuzi aliyedai kuwa Bw Odinga ndiye alishinda katika uchaguzi mkuu uliopita.
Lakini duru zinasema kuwa Bw Mbadi hajamsamehe Bw Odinga kwa kumlazimisha ajiondoe katika kinyang’anyiro cha ugavana wa Homa Bay mwaka jana ili ampishe Bi Gladys Wanga.
Hii ndio maana, kwa mfano, Bw Mbadi ameanzisha kumpiga vita Gavana Wanga kuhusiana na masuala kadha yanayohusu kaunti hiyo, kama vile malipo ya mishahara duni ya walimu wa chekechea.
Subscribe our newsletter to stay updated