NA MERCY KOSKEI
ALIYEKUWA mwigizaji wa Nairobi Diaries, Diana Clara Ojenge almaarufu Mishi Dorah amefunga pingu za maisha na mpenzi wake Mhindi.
Mishi Dora na mpenziwe Bohra walifunga ndoa katika sherehe ya siri ya kitamaduni iliyofanyika Little Gem Resort katika Kaunti ya Siaya Juni 3, 2023.
Katika video iliyosambazwa na mwigizaji Sandra Dacha, Mishi Dorah alionekana amevalia gauni jeupe la kitamaduni huku mumewe akivalia suruali nyeupe walipokuwa wakila kiapo mbele ya familia zao na marafiki.
Harusi hiyo yenye mada ya “dhahabu” iliyongozwa na mfawidhi mcheshi maarufu Eric Omondi.
Mwigizaji huyo wa zamani alimmiminia sifa mumewe, huku akielezea safari yao kama wanandoa kabla ya siku yao kubwa.
Alibainisha kuwa mume wake ni mwanamume kamili ambaye alivutia moyo wake na kuapa kutekeleza majukumu yake kama mke.
Kwa upande wake, Bohra aliapa kumpamba mke wake na upendo usio na masharti huku akiwashukuru wageni waliohudhuria sherehe hiyo.
Pia alielezea changamoto walizokumbana nazo katika mahusiano yao kabla ya kufunga ndoa huku akimhakikishia Mishi Dora kuwa ndoa yao itakuwa na furaha.