NA WANDERI KAMAU
MATAMSHI ya mwanawe Rais Yoweri Museveni wa Uganda, Jenerali Muhoozi Kanairugaba, kwamba huenda akaishabulia Kenya na kuiteka Nairobi kwa muda wa wiki mbili, yameibua vita baridi kati ya Urusi na mataifa ya Magharibi katika udhibiti wa siasa za Afrika Mashariki.
Muhoozi alitoa msururu wa jumbe hizo Jumanne kupitia mtandao wa Twitter, akisema kuwa yuko tayari kuliongoza jeshi la taifa hilo kuivamia Kenya na kuteka maeneo “yaliyokuwa yakimilikiwa na Uganda hapo awali.”
Ijapokuwa Rais Museveni aliomba msamaha kwa Rais William Ruto na Wakenya kwa jumla baadaye, wadadisi wa masuala ya mahusiano ya kimataifa wanasema kuwa kauli hizo hazipaswi kuchukuliwa kwa urahisi hata kidogo.
Kulingana na Dkt Geoffrey Musila, ambaye ni mhadhiri wa Siasa za Kimataifa, kauli ya Muhoozi inaashiria uwepo wa vita baridi kati ya Amerika na mataifa ya Magharibi kwa upande mmoja dhidi ya China na Urusi, kwenye mbio za kupata udhibiti wa kisiasa katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Kulingana na mdadisi huyo, hatua hiyo imechangiwa na mwelekeo mpya ambao Rais Ruto ameonekana kuchukua kisiasa; kujaribu kufufua urafiki kati ya Kenya na mataifa ya Magharibi.
Tangu 2003, ushawishi wa mataifa hayo ulianza kupungua nchini, baada ya Rais Mstaafu (marehemu) Mwai Kibaki, kubuni urafiki wa kisiasa na kiuchumi na China, hali iliyoziondoa Amerika na Uingereza kama washirika wakuu wa Kenya kisiasa na kimaendeleo tangu miaka ya tisini.
Kutokana na “urafiki” huo, Kenya ilifaidika pakubwa, baada ya China kuanzisha ujenzi wa miundomsingi muhimu kama barabara.
Baada ya Rais Kibaki kung’atuka uongozini mnamo 2013, Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta aliendeleza urafiki huo, ukimwezesha kupanua ujenzi wa barabara na miundomsingi mingine muhimu hadi alipoondoka uongozini mwaka huu 2022.
Wadadisi wanasema kuwa licha ya Kenya kufaidika pakubwa kimiundomsingi, urafiki kati yake na China ndicho chanzo cha zigo kubwa la deni la kimataifa linaloiandama Kenya na mataifa mengine barani Afrika kwa sasa.
“Bila shaka, moja ya malengo makuu ambayo ameonyesha Rais William Ruto ni kupunguza deni la kitaifa. Kwa upana, China ndiyo imekuwa ikilaumiwa pakubwa kwa kuongeza deni hilo. Hiyo ndiyo sababu ambayo imemfanya kuanza kurejesha na kufufua urafiki baina ya Kenya na mataifa ya Magharibi,” akasema Dkt Musila.
Anasema kuwa kinyume na Kenya, Uganda imeendelea kuwa mshirika mkuu wa China na Urusi, hilo likidhihirishwa na ziara aliyofanya majuzi, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Urusi, Sergei Lavrov, nchini Uganda.
“Ni wazi kuwa Urusi ni mshirika wa karibu wa Uganda. Mfumo wa uongozi wa Rais Museveni unalingana na ule wa Rais Vladimir Putin wa Urusi. Hawa ni viongozi wawili wenye misimamo mikali, hasa dhidi ya Magharibi,” akaeleza.
Kulingana na Prof Macharia Munene, ambaye pia ni msomi wa mahusiano ya kimataifa, moja ya sababu ambazo zimedhihirisha juhudi za Rais Ruto ni ziara alizofanya nchini Amerika na Uingereza mara tu baada ya kuapishwa.
Subscribe our newsletter to stay updated