NA CHRIS ADUNGO
MWALIMU anastahili kuwa mwepesi wa kumhimiza mwanafunzi kujitahidi katika safari ya elimu.
Awe karibu na wanafunzi ili ajue changamoto wanazopitia, awasaidie kadri ya uwezo wake na awaamshie hamu ya kuthamini masomo yote.
Haya ni kwa mujibu wa Bw Dennis Shonko ambaye sasa ni mwalimu katika shule ya msingi ya Enarupa Oongila, Kaunti ya Narok.
“Mwalimu bora achangamkie masuala yanayofungamana na mtaala na asome kutoka kwa vyanzo mbalimbali ili awe chemchemi ya maarifa kwa wanafunzi wanaomtegemea. Ajitahidi kuhudhuria vipindi vyote, awe mnyumbufu katika maandalizi ya vipindi na mbunifu katika uwasilishaji wa somo lake,” anasema.
Zaidi ya kuwa mwalimu, Shonko pia ni mwanateknolojia, mshairi shupavu na mwandishi chipukizi. Alizaliwa katika Kaunti ya Narok zaidi ya miaka thelathini iliyopita. Ndiye mwanambee katika familia ya watoto watano wa Bw Joshua Shonko na Bi Emily Shonko.
Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya Kwihota, Ruiru, Kaunti ya Kiambu. Akiwa darasa la nane, alijiunga na shule ya msingi ya Ilkirragarien, Narok. Alifaulu vyema na akajiunga na shule ya upili ya Olololulung’a, Narok.
Huko ndiko alikokutana na Bw Charles Wairegi (Mwalimu Mkuu) na Bi Caroline Wekesa waliompokeza malezi bora ya kiakademia na kumvuvia hamu ya kukichapukia Kiswahili.
Baada ya KCSE, Shonko alijiunga na Chuo cha Smart Media, Naivasha, kusomea Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. “Ninapenda kutumia maarifa yangu ya kiteknolojia katika ufundishaji. Hufurahi sana ninapowaona wanafunzi wangu wakielewa yote ninayowafunza kwa namna hii. Vifaa vya kidijitali ni muhimu sana katika utekelezaji wa Mtaala wa Umilisi (CBC),” anakiri.
Mnamo 2014, baada ya kufanya vibarua vya sampuli mbalimbali, Shonko alijiunga na Chuo cha Mafunzo ya Ualimu cha Murang’a hadi mwaka wa 2016. Alitangamana kwa karibu na waliokuwa wahadhiri wake, hasa Bw Mose, Bw Nyangweso na Bi Mogambi waliompa ilhamu ya kukithamini Kiswahili.
Haja ya kujiendeleza kitaaluma ilimpa msukumo wa kujiunga na Chuo Kikuu cha Kenyatta mnamo 2019 kusomea taaluma ya ualimu.
Baada ya kuhitimu kutoka Murang’a TTC, Shonko alianza kufundisha katika shule ya msingi ya Pink Roses, Kiambu. Alihudumu huko kwa kipindi cha miaka miwili kabla ya kuguria shule ya msingi ya Ridgesview, Naivasha.
Tume ya Huduma kwa walimu (TSC) ilimwajiri mnamo Januari 2020 na kumtuma kufundisha katika shule ya msingi ya Entashata, Kaunti ya Kajiado.
Zaidi ya kuandaa miswada mingi ya riwaya, tamthilia, hadithi za watoto na hadithi fupi, Shonko anajivunia pia kuchangia pakubwa safu za mashairi katika gazeti la Taifa Leo.
Amekuwa katika safari ya kukuza vipawa vya wanafunzi katika uandishi wa kazi bunilizi na za kitaaluma. Mbali na tamthilia ‘Wimbi la Mabadiliko’, ameandika pia novela ‘Mwisho wa Siri’ na hadithi fupi ‘Nguvu za Bahari’ katika antholojia ya ‘Baiskeli ya Babu na Hadithi Nyingine’.