Na CHRIS ADUNGO
MWALIMU hafai kuwa kiini cha wanafunzi wake kukata tamaa katika safari ya masomo.
Anastahili kujikusuru kufunza hadi mwanafunzi aelewe anachofundisha kikamilifu. Amwezeshe mwanafunzi kutambua na kutononoa vipaji vyake na amtie motisha ya kupenda vitabu – dafina iliyohifadhi maarifa na busara si haba.
“Vijana wa siku hizi ni wepesi wa kutumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii badala ya kusoma vitabu. Mustakabali wa usomaji wa vitabu uko hatarini. Walimu hatuna budi kuubadilisha mkondo huu ili taifa lisiangamie,” anasema Bw Mwinyi P. Kuria almaarufu Masharubu.
Usuli wake ni kitongoji cha Mukiri Tene, kata ya Nyakio-Kinangop, Kaunti ya Nyandarua. Alizaliwa 1988 akiwa kifungua mimba katika familia ya watoto watatu wa Bw Francis Maina na Bi Anna Wacuka.
Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya Bongo, Nyandarua (1995-2002) kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Kieni, Nakuru (2003-2004) kisha shule ya upili ya St Francis Subukia (2005-2006).
Kuria alisomea ualimu katika Chuo cha Kaimosi, Kaunti ya Vihiga (2007-2009). Aliyemchochea zaidi kujibwaga katika ulingo wa ualimu ni Guru Ustadh Wallah Bin Wallah. Ili kujitia makali zaidi, alijiunga na WASTA Kituo cha Kiswahili na Taasisi ya Taaluma ya Kiswahili mnamo 2010 na akahitimu kwa stashahada ya Kiswahili 2011.
Aliwahi pia kusomea Uhasibu hadi kiwango cha CPA-K. Kwa sasa anajiendeleza kitaaluma kwa kusomea Shahada ya Elimu (Kiswahili/Historia) katika Chuo Kikuu cha Mt Kenya (MKU). Kubwa zaidi katika maazimio ya Kuria ni kuwa Waziri wa Elimu katika siku za usoni.
Alianza kufunza katika shule ya Jacridge, Ruiru (2010) kabla ya kuhamia katika shule ya Joram G.M (2011-2012) kisha Makini Schools (2013- 2021). Kwa sasa ndiye Mkuu wa Idara ya Kiswahili katika shule ya Ruaraka jijini Nairobi.
Mkurugenzi wa Distinction Publishers, Bw Henry Mogoba, ndiye alitambua kipaji cha uandishi cha Kuria na akamchochea aanze kuvuvia umma busara, maarifa na ujuzi wake kupitia sanaa ya utunzi.
Baadhi ya kazi zake zilizochapishwa ni ‘Mentor Insha Elekezi’, ‘Mentor Kielekezi (Gredi 4)’, ‘Distinction Kipeo cha Lugha (Gredi 5, 6, 7)’, ‘Superbrain Ufunguo wa KCPE’, ‘Distinction Utendeti wa Chambuzi za KCPE’, ‘Distinction Ensaiklopidia’ na ‘Distinction Ubashiri wa KPSEA’.
Mingi ya miswada yake iko katika hatua za mwishomwisho za uhariri katika kampuni na mashirika mbalimbali ya uchapishaji wa vitabu humu nchini.
Ili kuitetea na kukuza zaidi lugha ashirafu ya Kiswahili, Kuria ana chaneli ya YouTube, ‘Masomo Mtandaoni’.
Vilevile, ni mtahini wa kiwango cha kitaifa na mkuza mitaala. Isitoshe, ni mhamasishaji stadi wa Kiswahili katika shule anuwai kupitia warsha na makongamano ya lugha.
Anaamini kuwa familia ni msingi wa ufanisi maishani. Kwa pamoja na mkewe, Bi Angeline N. Kimani (Selina), wamejaliwa watoto wawili – Annet Wacuka na Fabian Maina.
Subscribe our newsletter to stay updated