Na MARGARET MAINA
Muda wa kuandaa kabla ya kuoka: Saa mbili
Muda wa kuoka: Dakika 40
Walaji: 4
Vinavyohitajika
Unga wa ngano 1 kilo
Hamira ya chenga vijiko 2
Maziwa kikombe ¼
Maji kikombe ¼
Chumvi kijiko 1 cha chai
Sukari vijiko 3
Siagi vijiko 2
Maelekezo
Chemsha maji kiasi halafu tia maji ya ufufutende kwenye hamira.
Ongeza sukari huku ukikoroga. Acha kwa dakika 15 hadi uone povu.
Weka mchanganyiko wa hamira, maji na sukari kwenye bakuli kubwa. Ongeza hapo maziwa ya moto kiasi, siagi iliyoyeyushwa halafu ongeza unga kidogokidogo huku ukikoroga.
Ukiona unga unaanza kunata, hamishia donge kwenye ubao wa kukandia.
Kanda kwa dakika 10 mpaka uone kwamba unapolibonyeza donge, linajirudisha.
Weka donge kwenye bakuli na ufunike na kitambaa safi. Acha unga huo wa donge uumuke kwa muda wa saa moja.
Baada ya saa moja, toa donge na uliweke kwenye ubao. Chukua msukumio usukume donge lote kisha kunja kama mkate.
Weka donge lenye shepu ya mkate kwenye chombo cha kuokea. Funika tena na acha uumuke tena kwa muda mwingine wa saa moja.
Washa ovena na uacha ipate moto kwa dakika 10 kwa nyuzijoto za 180 katika kipimo cha sentigredi.
Oka mkate kwenye ovena kwa dakika 30.
Toa mkate na ubrashi na siagi iliyoyeyushwa juu ya mkate. Rudisha kwenye ovena kwa muda wa dakika mbili kisha toa.
Mkate upo tayari.