NA ENOCK NYARIKI
AKILI za Katiti zilisuka kwa haraka jibu ambalo angempa baba yake na ambalo lingemfanya kumeza joto alilokuwa nalo asubuhi ile.
Makopo alishtua kichwa chake upande na kungoja Katiti ambaye alikuwa amesimama kujielezea.
“Nguo zetu za kuvaa kuenda kanisani siku ya Jumapili ni chafu, baba,” Katiti alisema.
“Katiti!’’ Makopo aliita kwa sauti nzito na imara.
“Naam baba,’’ Katiti aliitika.
“Kufua nguo ni wajibu wa nani?’’ Makopo alifuatisha kwa swali.
“Ni wetu baba,’’ Katiti alijibu kwa unyenyekevu.
“Halafu?”
Kila wakati Bwana Makopo alipotamka kauli halafu bila kuifuatisha kwa maneno mengi, hiyo ilikuwa ishara kwamba hasira zake zilikuwa zimefikia kiwango mchemko. Katiti na ndugu zake walinyamaza kama kwamba walikuwa wamenyang’anywa ndimi.
Bwana Makopo alitoa amri: “Kila mmoja achukue mtungi wa lita tano!’’
Vijana walitii amri. Walitakiwa kulijaza pipa la lita mia moja lililosimama kwenye varanda nje ya nyumba yao.
Maji yenyewe walikuwa wayateke kutoka mtoni; umbali wa kilomita moja kutoka nyumbani kwao.
Jua la utosini liliwachoma vichwa na majasho kuwatiririka kutoka vipajini kwenda mashavuni walipokuwa wakivikwea vilima vya Masosa huku wameibeba mitungi ya maji.
Walifanikiwa kulijaza lile pipa wakati jua lilipokuwa likiaga miti. Jukumu jingine lilikuwa kuzifua nguo zao mpaka zitakate.
Jumapili iliyofuata, hakuna hata mtoto mmoja aliyetaka kusalia nyumbani. Wote walijiandaa asubuhi na mapema kuenda kanisani.
Adhabu waliyopewa na baba yao wiki iliyokuwa imetangulia iliwafanya kushika sikio.
Ama kweli, ukipigao ndio ukufunzao.
Subscribe our newsletter to stay updated