NA SAMMY WAWERU
RAIS William Ruto alichelewa kuwasili katika Uwanja wa Moi, Embu ambako maadhimisho ya Madaraka Dei 2023 yanafanyika, Alhamisi, Juni 1.
Dkt Ruto anaongoza taifa kuadhimisha Sikukuu hii ya Juni 1 kila mwaka, inayoandaliwa kusherekea Kenya kupata uhuru wa ndani kwa ndani kujitawala kutoka kwa serikali ya Mbeberu 1963.
Kinyume na itifaki za sherehe za kitaifa, ambapo kiongozi wa nchi anapaswa kuwasili uwanja wa hafla kabla ya saa nne na nusu asubuhi, Rais Ruto alifika Uwanja wa Moi baada ya saa tano.
Alikabirishwa na naibu wake, Rigathi Gachagua, akiwa kwenye gari maalum la kikosi cha majeshi ya Kenya (KDF) huku akiandamana na Mkuu wa Majeshi Meja Jenerali Francis Omondi Ogolla.
Baadaye, alikagua gwaride la heshima la wanajeshi.
Kenya inaadhimisha miaka 60, baada ya kupata uhuru wa kujitawala ndani kwa ndani kutoka kwa mkoloni.