• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
SOKOMOKO WIKI HII: Sabina akaangwa na Wakenya kwa kuhoji maombi bungeni

SOKOMOKO WIKI HII: Sabina akaangwa na Wakenya kwa kuhoji maombi bungeni

NA CHARLES WASONGA

MBUNGE maalum Sabina Chege Alhamisi alijipata pabaya alipoelekezewa cheche za lawama na Wakenya mitandaoni kwa kulalamikia idadi kubwa ya viongozi wa kidini walioongoza maombi wakati wa kikao cha pamoja Bunge la Kitaifa na Seneti.

“Nasikia watu wengine wakilalamika tunamhusudu Mungu kisiasa. Lakini tumekuwa tukimtukuza shetani kwa muda mrefu zaidi. Sabina Chege acha Mungu atawale bungeni na asasi zote za serikali!” Seneta wa zamani Isaac Mwaura akasema kupitia Twitter.

Wakenya wengine walimkaripia Bi Chege wakimtaka kuomba msamaha “kwa Mungu kwa kutotambua ukuu wake.”

Viongozi watano wa kidini waliongoza kipindi cha maombi kabla ya Rais William Ruto kuhutubia kikao hicho cha kwanza cha Bunge la 13.

Ilikuwa hotuba yake ya kwanza tangu kuapishwa kwake kuwa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Kenya mnamo Septemba 13 mwaka huu.

Lakini kwa mtazamo wa Bi Chege haikuwa ‘kawaida’ kwa jumla ya viongozi watano wa kidini kuongoza kipindi cha maombi na hivyo kudumu “kwa dakika nyingi zaidi”.

“Kwa mara ya kwanza tumewaona viongozi wengi wa kidini wakija bungeni na kipindi cha maombi kimekuwa kirefu zaidi.

Nadhani tumevuka mipaka; lakini sipingi maombi kwani mimi ni mcha Mungu. Nadhani tunahitaji kudhibiti suala hili,” Bi Chege akawaambia wanahabari baada ya Dkt Ruto kukamilisha hotuba yake.

Kulingana na mbunge huyo, ingekuwa bora kwa uongozi wa Bunge kualika viongozi wawili wa kidini; Mkristo na Mwislamu kama zamani.

You can share this post!

Wolves wamtimua kocha Bruno Lage kutokana na msururu wa...

KIGODA CHA PWANI: Teuzi za Jumwa, Mvurya zaleta mkondo mpya...

T L