NA PATRICK KILAVUKA
USIJE ukadunishwa na yeyote unapofanya kitu au kuwa mwoga.
Kuwa mkakamavu na usiyekata tamaa! Isitoshe, maneno ya watu ni upepo uvumao usiohitaji kuuweka katika kilindi cha roho yako yasije kukatiza ndoto zako!
Kuwa ngoi kunamhitaji mhusika kuwa tayari kuwaelekeza wenzake katika safari ya kuimarisha vipaji au talanta zao. Ngoi anafaa kuwa jasiri katika kuongoza kikundi kwani endapo tu atateleza basi jahazi la kikundi cha uimbaji huwa tayari kupoteza mwelekeo.
Hayo ni kwa mujibu wa kiongozi wa nyimbo Peace Chaviva, 11, ambaye hushika hatamu za kikundi cha waimbaji cha shule ya msingi ya Eunice Preaparatory, kaunti ndogo ya Dagoretti Kusini, Kaunti ya Nairobi.
Anakariri kwamba silaha ya ngoi ni uwezo wa kuwa imara jukwaani na kuimba kwa weledi uwe unajua wimbo unaouongoza kwa undani, uwe wa kabila lako au la!
Kuwa mwepesi kunasa nyimbo na kukariri kumemfanya mwalimu Lucy Abukui ambaye amemfinyanga kuwa ngoi mwaka huu kuamua kwamba atashika usukani wa kuongoza kikundi cha waigizaji kushiriki katika mashindano.
“Ni chini tu ya wiki baada ya kuandaliwa na ameweza kuumanya wimbo wa Kiteso na kuwapeleka wengine jukwaani,” anasema mwalimu huyo.
Wameshiriki katika mashindano ya tamasha za drama za shule za msingi za kaunti ndogo ya Dagoretti Kusini ambayo yaliandaliwa katika shule ya msingi ya Kinyanjui na kufanya vizuri licha kwamba ilikuwa mara yake ya kwanza kufanya hivyo.
Yeye ni mwana wa pili katika familia ya watoto watatu wa familia ya Bi Eglay Kiarie na Bw Christopher Kiarie.
Kiu ya kuwa kiongozi wa nyimbo ilianza akiwa na miaka sita katika gredi ya kwanza.
Darasani ni mwerevu mithili ya Simba. Pia, kuwa machachari katika kufanya mambo kwa njia ya ufasaha kumeborsha uwezo wake.
Anasema kile kilimchochechea ni ujifunzaji kutoka kwa mtangulizi wake ngoi Mitchel ambaye ni jirani yake mtaani.
Ustadi wake kuongoza nyimbo, uliinuka zaidi pale alipotambua kwamba ukitaka kufaulu katika kila nyanja, lazima ukope mawazo na kuyaweka katika mazoezi pamoja na kujifunza mapya.
Mbali na kuongoza nyimbo, yeye pia hukariri mashairi kanisani Green Pastures Tabernacle, Mutuini na shuleni kwenye gwaride na hafla mbalimbali.
Anasema kwamba katika maisha yake ya halafu, angependa kuwa daktari wa upasuaji kwani sasa anazamia katika masomo ya Hisabati, lugha na sanyansi kujizolea maarifa ya kitaaluma.
Aidha, amelikumbatia somo la muziki kukuza ujuzi wake wa uimbaji na angependa kuwa ngoi hadi amalize shule.
Changamoto yake imekuwa kusawazisha muda wa masomo na talanta lakini kwa usaidizi wa mwalimu wake, amefaulu kuwa na wakati wa kufanya kila kitu kwa wakati wake.
Yeye humakinika wakati wa ratiba ya masomo na kutumia wakati mwingine kufanya mazoezi.
Uraibu wake ni kusakata densi na kupika.
Subscribe our newsletter to stay updated