NA WANDERI KAMAU
IMEIBUKA kuwa dalili za mrengo wa Kenya Kwanza kupanga mageuzi ya Katiba ili kumwezesha Rais William Ruto kuendelea kuhudumu kama rais hata baada ya mihula yake miwili kukamilika, zilianza kudhihirika kitambo.
Wadadisi wa siasa wanasema kauli ya mbunge Salah Yakub (Fafi) kuwa wabunge wa mrengo huo wanajadili kuhusu mikakati ya kugeuza katiba ili kumwezesha Rais Ruto kuwania urais kwa mihula miwili zaidi, ni kutimia kwa juhudi ambazo zimekuwa zikiendelea tangu Rais alipoapishwa.
Kulingana nao, ishara ya kwanza ilikuwa hatua ya Rais Ruto “kuwanyakua” wabunge 10 waliochaguliwa kama wawaniaji huru na kuwarai kuunga mkono muungano huo.
Kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Agosti 9, jumla ya wabunge 12 walichaguliwa kama wawaniaji huru.
Wabunge hao walitangaza kuunga mkono Kenya Kwanza baada ya kuungana na wabunge wa mrengo huo kwenye kikao cha kwanza walichofanya na Rais Ruto mara tu baada ya kuapishwa kwake.
“Tunawashukuru ndugu zetu (wabunge huru) kwa kukubali kuwa sehemu ya familia ya Kenya Kwanza,” alisema Rais Ruto.
Baadaye, Rais Ruto aliwakaribisha wabunge saba zaidi kutoka chama cha United Democratic Movement (UDM) kinachoongozwa na Seneta Ali Roba (Mandera).
Ijapokuwa chama hicho kilikuwa katika muungano wa Azimio la Umoja, viongozi wake walidai kuwa walishinikizwa kujiunga na mungano huo “shingo upande”.
“Tumetangaza ushirikiano mpya na Kenya Kwanza. Lengo letu ni kuhakikisha tuko katika nafasi tutakayohakikisha watu wetu wanafaidika kutoka kwa serikali iliyo uongozini,” akasema Bw Roba, alipokutana na Rais Ruto.
Ishara ya tatu ni hatua ya Rais Ruto “kuvamia” ngome za kisiasa za kiongozi wa Azimio, Bw Raila Odinga, na “kunyakua” baadhi ya wabunge waliokuwa wakimuunga mkono.
Hilo lilidhihirishwa na hatua ya mbunge David Ochieng (Ugenya) kuwaongoza wanasiasa kadhaa kutoka eneo la Nyanza kutangaza “safari mpya” ya kisiasa kwa kumuunga Rais Ruto. Mbunge huyo alichaguliwa kwa tiketi ya chama chake cha Movement for Democracy and Growth (MDG).
Mbali na hayo, wanasiasa wengine kutoka Nyanza, wakiongozwa na aliyekuwa gavana wa Nairobi, Dkt Evans Kidero, aliyekuwa mwaniaji ugavana katika Kaunti ya Siaya, Nicholas Gumbo, pia walitangaza kumuasi Bw Odinga na kuanza kumuunga Dkt Ruto.
“Mielekeo hii inadhihirisha kuwa juhudi hizi zilianza kitambo, hivyo matamshi ya Bw Yakub ni sauti tu kuhusu mipango ambayo imekuwa ikiendeshwa faraghani bila ufahamu wa watu wengi,” asema Bw Oscar Plato, ambaye ni mdadisi wa siasa.
Anasema kwa kuungwa mkono na wabunge wengi, hilo ndilo lililoiwezesha Kenya Kwanza kushinda nafasi za Uspika katika Bunge la Kitaifa na Seneti mtawalia.
Hili ni kupitia kuchaguliwa kwa Moses Wetang’ula na Bw Amason Kingi kama maspika wa Bunge na Seneti mtawalia.
Mdadisi huyo anasema kuwa upeo wa juhudi hizo ni hatua ya mrengo huo kutangaza kuwa vyama vyote tanzu katika Kenya Kwanza vitavunjwa ili kujiunga na UDA.
“Kikweli, baada ya tangazo hilo, baadhi ya vyama, kama vile Chama cha Kazi (CCK) chake Waziri wa Biashara na Viwanda Moses Kuria vilitangaza notisi ya kuvunjwa,” akaeleza.
Kulingana naye, hilo ni dhihirisho tosha kuwa kwa kuchukua udhibiti wa taasisi muhimu kama Seneti na Bunge la Kitaifa, haitakuwa vigumu kwa Rais Ruto kushinikiza mageuzi ya kikatiba ili kumwongezea mamlaka na muda wa kuhudumu.
Hata hivyo, washirika wa Rais Ruto wanataja kauli ya mbunge huyo kuwa “maoni yake binafsi” wala hawana mpango kama huo.
“Hayo ni maoni yake binafsi. Kenya Kwanza ni mrengo unaomruhusu kila mmoja kujieleza,” asema Seneta Samson Cherargei (Nandi).
Subscribe our newsletter to stay updated