NA SAMMY WAWERU
VIUNGO maalum vya nyama za mifugo, vimethibitisha kuteka masoko yenye ushindani mkuu ndani na nje ya nchi.
KenMeat, mojawapo ya kampuni inayouza bidhaa zake ng’ambo inakiri sehemu mbalimbali za nyama zikiongezwa thamani na kupakiwa ni kitega uchumi cha haraka.
“Sisi ni ‘wataalamu’ wa mseto wa viungo vya nyama za mifugo, tunazouza nje ya Kenya,” asema Caroline Itotia, Msimamizi Kitengo cha Mauzo na Soko katika kampuni hiyo iliyoko Athi River.
Kulingana na afisa huyo, KenMeat ina soko tayari ya bidhaa zake, nchi za Mashariki ya Kati Uarabuni.
Soko jingine ni Barani Afrika, hasa nchini Somalia na Sudan.
Viungo ambavyo kampuni hiyo imeegemea kwavyo ni pamoja na sirloin chuck, rib, sirloin steak, ram steak, briskets, shanks, flank, leg, breast na shoulder.
“Tunahudumu na wafugaji kati ya 800 – 1, 000,” Caroline adokeza.
Afisa huyo aidha anafichua kwamba kwa siku huchinja idadi jumla ya mifugo 7, 000, hiyo ikiwa ni kondoo na mbuzi.
Wanyama wakubwa, ndio ng’ombe, huchinja kati ya 200 – 300 kwa siku.
Caronile anaambia Akilimali Dijitali kwamba, nyama zilizoongezwa thamani zinateka soko bora zaidi.
“Tunapoongeza nyama thamani kwa kusindika (processing), mapato ni ya juu kiasi cha kulazimika kuagiza mifugo nje ya nchi kuziba gapu iliyopo.”
Bidhaa zilizoongezwa thamani za kampuni hiyo ni pamoja na; soseji, soseji ya Kiafrika – mutura, beef Vienna, burgers na meatballs.
“Tuna aina 50 hadi 60 ya bidhaa za nyama zilizosindikwa,” Caroline akafichua wakati wa mahojiano.
KenMeat, ilikuwa miongoni mwa kampuni, mashirika na wadauhusika walioshiriki Maonyesho ya Nyama Kenya 2023 yaliyofanyika ukumbi wa KICC, Nairobi.
Maonyesho hayo yalikuwa makala ya pili, yaliyoandaliwa na Shirika la Habari la Nation, kwa ushirikiano na Wizara ya Kilimo na Mifugo, na wadauhusika wengine katika mtandao wa uzalishaji nyama.
“Tunasambaza bidhaa zilizoongezwa thamani kwa maduka mbalimbali ya kijumla nchini.”
Kuziba upungufu wa mifugo, KenMeat ina mpango kuanzisha ranchi za malisho na kualika wafugaji wateja wake.
Kulingana na Caroline, ni mradi ambao unatarajiwa kuleta mageuzi katika malengo ya kampuni hiyo kusaidia katika mtandao wa uzalishaji nyama nchini.