• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
WARUI: Tuzo ya Nobel ya Abdulrazak ushindi kwa elimu Afrika

WARUI: Tuzo ya Nobel ya Abdulrazak ushindi kwa elimu Afrika

Na WANTO WARUI

KWA mara nyingine tena tuzo inayoenziwa sana kote ulimwenguni imerudi katika eneo letu la Afrika Mashariki mara hii katika sekta ya elimu kwa Mtanzania Abdulrazak Gurnah.

Gurnah, mwenye umri wa miaka 72 ameshinda tuzo hiyo kutokana na uandishi wake wa fasihi usiyotetereka juu ya masuala ya ukoloni na ukimbizi.

Mnamo 2007, mwandishi Doris Lessing kutoka Zimbabwe alishinda tuzo hiyo akiwa mwandishi wa pili Mwafrika baada ya Mnaijeria Wole Soyinka aliyeshinda mwaka wa 1986.

Itakumbukwa pia, hayati Profesa Wangari Maathai kutoka Kenya alishaweza pia kujishindia tuzo hiyo ya Nobel kutokana na bidii yake ya kulinda na kutetea mazingira.

Mwandishi Gurnah, licha ya kwamba ana makao yake nchini Uingereza ameiweka Afrika Mashariki katika ramani ya wasomi na waandishi mashuhuri wenye elimu na uandishi wa kina.

Katika vitabu vyake kumi vya riwaya alivyoandika, ameonyesha msisitizo na mapenzi makubwa ya uandishi huku akidhihirisha wazi matokeo hasi ya ukoloni na athari za ukimbizi kwa jamii zinazohusika.

Gurnah, ambaye ameandika vitabu kama vile Paradise ameonyesha ukakamavu mkubwa katika kukosoa sera mbaya za ukoloni ambazo athari zake zinasikika miaka mingi baadaye.

Abdulrazak ni mwandishi maarufu kutoka eneo hili, licha ya kuwa anaadika kwa lugha ya Kiingereza.

Alitoka huku Afrika kama mkimbizi katika miaka 1960 kutokana na mateso yaliyokuwamo dhidi ya watu wenye asili ya Kiarabu chini ya utawala wa aliyekuwa rais wa Zanzibar Abeid Karume.

Tangu wakati huo, hakuweza kurudi tena ila tu mwaka wa 1984, alipomtembelea baba yake huko Unguja kabla ya kifo chake.

Kuchaguliwa kwake kwa tuzo hii kunakuja ambapo ulimwengu umeingia katika mtafaruku mkubwa wa wakimbizi kutokana na vita, njaa na siasa.

Tuzo hii ya Nobel ya Abdulrazak inaliweka eneo hili mbele na ni ishara nzuri kwa waandishi wengi wazuri kutoka Afrika Mashariki.

Eneo hili linajivunia waandishi mashuhuri wa vitabu baadhi yao wakiwa marehemu Shaaban Robert, John Ruganda, Euphrase Kezilahabi na Ken Walibora.

Aidha, orodha ya waandishi walioko sasa ni ndefu sana wakiwa ni pamoja na Shafi Adam Shafi, Ngugi wa Thiong’o, Charles Lubega, Mohamed Said miongoni mwa wengine wengi.

Huu ni motisha mkubwa kwa waandishi wakongwe wa Afrika Mashariki ambao wanaendelea kuandika ama wale ambao kazi zao tayari zinasomwa pamoja na waandishi wachanga wanaoingia katika sekta hii ya uandishi wa vitabu.

Hakuna shaka kuwa elimu inayotolewa katika shule na vyuo vyetu ina uwezo mkubwa wa kukabiliana na matatizo ya bara hili na ulimwengu kwa ujumla.

You can share this post!

Wachungaji waomba amani idumu Kenya inapojiandaa kwa...

ONYANGO: Mchujo ufanywe siku moja kubana nje wanaorukaruka

T L