• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 11:55 AM
WASONGA: Chiloba, wenzake wasaidie IEBC kufanikisha kura 2022

WASONGA: Chiloba, wenzake wasaidie IEBC kufanikisha kura 2022

Na CHARLES WASONGA

UTEUZI wa waliokuwa maafisa wanne wa ngazi za juu katika Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kushikilia nyadhifa kuu katika asasi zitakazohusika na uchaguzi mkuu wa 2022 ni mtihani mkubwa kwao.

Ezra Chiloba, Emmaculate Kassait, James Muhanji, na Anne Nderitu watahitaji kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na weledi mkubwa ili kuondoa lawama zilizoelekezwa kwao kuhusiana na dosari zilizokumba chaguzi za 2013 na 2017, waliposhikilia nyadhifa za juu katika IEBC.

Bw Chiloba, ambaye alikuwa Afisa Mkuu Mtendaji wa tume hiyo, ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Mawasiliano Nchini (CA).

Anatarajiwa kutekeleza wajibu mkubwa katika uchaguzi huo kwa sababu asasi hiyo inatwikwa jukumu la kuhakikisha kuna mawasiliano ya masafa ya 3G na 4G katika vituo vyote vya kupiga kura nchini na hivyo kuiwezesha IEBC kutuma, haswa matokeo ya uchaguzi wa urais hadi kituo cha kitaifa cha ujumuishaji bila matatizo yoyote.

Tayari mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati amelalamika kuwa kuna maeneo ya humu nchini ambayo hayajafikiwa na masafa ya 3G ambayo watategemea kupeperusha matokeo ya uchaguzi.

Ikumbukwe kwamba hitilafu katika upeperushaji wa matokeo ya uchaguzi wa urais kutoka jumla ya vituo 11,500 vya upigaji kura ndio mojawapo ya sababu zilizochangia kufutiliwa mbali kwa matokeo ya uchaguzi wa urais mnamo 2017.

Hatua hiyo ilitumbukiza taifa hili katika lindi la taharuki ya kisiasa na hasara baada ya IEBC kuamuriwa irudie uchaguzi wa urais.Naye aliyekuwa Mkurugenzi wa Elimu kwa Wapigakura katika IEBC Emmaculate Kassait ambaye aliteuliwa kuwa Kamishna wa Data Novemba 2020, anasimamia data muhimu kuhusu uchaguzi mkuu kama vile idadi ya watu nchini.

Ni wajibu wa Bi Kassait kuhakikisha kuwa data zote kuhusu Wakenya ni salama na haziingiliwi wala kuvurugwa kwa njia yoyote.

Kwa upande mwingine, aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) katika IEBC James Muhati ndiye Afisa Mkuu Mtendaji wa Huduma Kenya.

Katika idara hii, Bw Muhati anasimamia miongoni mwa mengine data zilizoko katika stakabadhi za utambulisho kama vile vitambulisho vya kitaifa vitakavyotumika katika shughuli za usajili wa wapiga kura wapya unaoanza leo na upigaji kura mnamo Agosti 9, 2022.

Kwa upande wake Bi Anne Nderitu ambaye zamani alihudumu kama afisa wa mafunzo kuhusu Masuala ya Uchaguzi katika IEBC ndiye Msajili wa Vyama vya Kisiasa.

Afisi yake ina wajibu mkubwa katika uchaguzi mkuu ujao kwa sababu ndiyo inasajili vyama vipya na kuidhinisha miungano ya kisiasa.

Miungano hiyo ambayo inaendelea kubuniwa itakuwa kiunga muhimu katika kuamua mgombeaji wa urais atakayeshinda katika uchaguzi.

Bi Nderitu pia ndiye anasimamia orodha ya wanachama wa vyama vya kisiasa na ambayo itatumika katika michujo ya vyama hivyo kuelekea uchaguzi huo mkuu.

Kwa hivyo, kwa mtazamo wangu, ufanisi wa uchaguzi mkuu ujao utategemea zaidi utendakazi wa maafisa hawa wanne ambao zamani walihudumu katika IEBC.

Japo wengine wao walielekezewa lawama kuhusiana na dosari mbalimbali zilizotokea walipokuwa wakihudumu katika tume hiyo, sasa wanayo nafasi ya kujitakasa kwa kufanya kazi mzuri katika asasi hizi muhimu wanazozisimamia wakati huu.

You can share this post!

Hofu muda wa NMS ukielekea kumalizika

Firat atatangaza kikosi cha Harambee Stars kusafiri Morocco...