• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:55 PM
WASONGA: Vijana wahimizwe kujisajili kwa miradi ya kuwanufaisha

WASONGA: Vijana wahimizwe kujisajili kwa miradi ya kuwanufaisha

Na CHARLES WASONGA

NI jambo la kusikitisha kuwa ni wakati kama huu ambapo uchaguzi mkuu unakaribia ndipo wanasiasa wametambua umuhimu wa vijana katika taifa hili.

Wanasiasa hao, haswa wale wanaotaka kiti cha urais, wamekuwa wakitumia majukwaa mbalimbali kuwahimiza vijana kujitokeza kwa wingi kujisajili kuwa wapiga kura ili washiriki uchaguzi mkuu wa 2022.

Hii ni kwa sababu inakadiriwa kuwa kati ya wapiga kura wapya 6.3 milioni ambao Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inalenga kusajili, 5.2 milioni ni vijana ambao walitimu umri wa miaka 18 kati ya 2017 na sasa.

Idadi hii ni muhimu zaidi katika kuamua mshindi katika uchaguzi wa urais katika uchaguzi huo utakaofanyika mnamo Agosti 9, 2022.

Lakini wanasiasa hawa wamedhihirisha ubinafsi katika miito yao kwa vijana wajiandikishe kuwa wapiga kura.

Hii ni kwa sababu sijawasikia wanasiasa wanaowahimiza vijana kujitokeza kwa wingi kuwania nyadhifa mbalimbali katika uchaguzi huo.

Sijawahi kuwasikia Naibu Rais William Ruto, Kiongozi wa ODM Raila Odinga, Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper) na wengine wanaomezea mate kiti cha urais wakiwahimiza vijana kuwania viti katika uchaguzi huo.

Hii ina manaa kuwa wanasiasa hawa wanawachukulia vijana katika watu ambao wajibu wao ni kuwapigia kura pekee na wala sio watu wanaostahiki kushikilia nyadhifa za uongozi.

Huu ni ubinafsi mkubwa.

Vijana wanafaa kushikilia nyadhifa za uongozi ili waweze kushiriki katika mpango wa utungaji sera na maongozi ya taifa hili.

Hii ni kwa sababu wao ndio huathirika pakubwa na makali ya uongozi mbaya kizazi cha sasa cha viongozi, hali ambayo imechangia wengine wao kupotoza matumaini maishani.

Ningehimiza kwamba huku wanasiasa wanapowahimiza vijana kujitokeza kwa wingi wajiandikishe kuwa wapiga kura, pia wawahimize kujiandikisha katika mipango ya serikali inayolenga kuboresha maisha yao.

Kwa mfano, vijana wahimizwe na waelekezwe kujiandikisha katika mipango ya kuwapa nafasi za ajira kama vile; Kenya Youth Employment Opportunities (KYEOP), Ajira Digital Youth Empowerment Programmes (ADYED), Presidential Digital Talent Development Youth Programmes, miongoni mwa mingine.

Mipango kama hii, inayodhaminiwa na serikali kuu, ndio inaweza kuwasaidia vijana kujiendeleza kimaisha kando na kujiandikisha kuwa wapiga kura.

Wanasiasa wakome kuendeleza dhana kwamba umuhimu wa vitambulisho vya kitaifa kwa vijana ni katika kushirikisha shughuli za kisiasa pekee.

Vijana, haswa wale wanaoishi mashambani, watambue kuwa wanaweza kutumia stakabadhi hizo za utambulisho kwa shughuli nyingine nyingi za kuboresha maisha yao kando na kupiga kura.

You can share this post!

Vilio serikali inunue mifugo iliyo hatarini

‘Corona’ ya punda yalipuka na kuzua hofu kubwa...