• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
CHARLES WASONGA: Serikali iandame wanaokwepa ushuru badala ya kulemaza raia na mzigo zaidi

CHARLES WASONGA: Serikali iandame wanaokwepa ushuru badala ya kulemaza raia na mzigo zaidi

NA CHARLES WASONGA

KUNA msemo wa kale kwamba kuna vitu viwili pekee ambavyo ni lazima maishani: kifo na ushuru.

Japo ushuru ni mzigo wa kifedha kwa walipaji, ni wajibu muhimu kwa kila mwananchi.

Sababu ni kuwa serikali hutumia ushuru kufadhili huduma na miradi yote ya umma.

Miongoni mwa shughuli zinazofadhiliwa na pesa za ushuru ni usalama, elimu, afya, miundomsingi kama vile barabara, idara za kukabili majanga pamoja na uendeshaji kila siku wa wizara, idara na mashirika ya serikali.

Serikali pia hutumia ushuru kulipa mishahara ya watumishi wa umma, ambao ndio watekelezaji wa sera na ajenda zake.

Chini ya kivuli hiki Mswada wa Fedha 2023, ambao unatoa mwongozo kuhusu mpango wa serikali wa kuhusu utozaji ushuru ni muhimu zaidi katika utekelezaji wa ajenda za serikali hii ya Kenya Kwanza.

Utekelezaji wa mipango ya ushuru iliyoratibiwa katika mswada huu ndio utaiwezesha serikali ya Rais William Ruto kutekeleza bajeti yake ya kwanza ya kima cha Sh3.6 trilioni.

Lakini baada ya mswada huo kuletwa bungeni wiki jana, Wakenya wa matabaka mbalimbali walianza mara moja kulalamikia mapendekezo yaliyomo, yanayolenga kuongeza aina mbalimbali za ushuru na kuanzisha zingine mpya kama ule wa nyumba.

Pendekezo la kuongezwa kwa ushuru wa thamani (VAT) wa mafuta kutoka asimilia 8 hadi asilimia 16, limepingwa kwa sababu litachangia kupanda kwa gharama ya maisha.

Aidha, pendekezo kwamba watumishi wa umma wanaokula mshahara wa Sh500,000 kwenda juu walipe ushuru wa mapato (PAYE) wa asilimia 35 limepingwa na wengi.

Kwa mtazamo wangu badala ya serikali kupandisha viwango vya ushuru, inapaswa kupanua mawanda ya ulipaji kwa kuwaandama wakwepaji ushuru.

Hii ndio njia ya kipekee itakayoiwezesha serikali kukusanya ushuru wa kima cha Sh3trilioni kufikia mwisho wa mwaka wa kifedha wa 2023/2024, alivyoahidi Rais Ruto.

  • Tags

You can share this post!

Raila kortini kupinga jopo la Shakahola

Bonge la mechi AC Milan dhidi ya Inter Milan nusu fainali...

T L