• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:55 AM
MARY WANGARI: Mauaji ya Tirop ni uhalisia mchungu wa janga la dhuluma

MARY WANGARI: Mauaji ya Tirop ni uhalisia mchungu wa janga la dhuluma

Na MARY WANGARI

WINGU la majonzi liligubika Kenya wikendi wakati nyota mchanga wa Olimpiki, Agnes Tirop, alipopumzishwa nyumbani kwao Mosoriot, Kaunti ya Nandi.

Jamaa, marafiki na wanariadha wenza walimiminika kumuaga buriani bingwa huyo mwenye umri wa miaka 25 katika siku ambayo kwa kinaya, alistahili kusherehekea siku ya kuzaliwa kwake.Mshindi huyo chipukizi wa medali ya shaba katika mashindano ya duniani, alipatikana akiwa ameuawa kwa kudungwa kisu nyumbani kwake Iten, ambapo mumewe Ibrahim Rotich almarufu Manuu, ndiye mshukiwa mkuu.

Hata kabla ya Wakenya kujifuta machozi kwa kumpoteza barobaro huyo aliyekuwa mwingi wa matumaini kuhusu siku za usoni, ripoti kuhusu mauaji ya mwanariadha mwingine kwa jina Edith Muthoni, ziligonga vyombo vya habari.

Kifo cha mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 27 katika Kaunti ya Kirinyaga, vilevile kilihusishwa na mumewe Kennedy Kamau.Visa hivi vya kuhuzunisha ni baadhi tu ya mauaji ya kikatili baina ya wanandoa kote nchini hali ambayo imeangazia kero la dhuluma za kinyumbani.

Takwimu mpya nchini zinaonyesha uhalisia wa kutisha wa dhuluma za kinyumbani huku idadi kubwa ya wahasiriwa wakiwa wanawake.Si ajabu baadhi ya watu wamekuwa wakitania kuwa, njia mojawapo ya kuaga dunia upesi zaidi ni kwa kujiingiza katika ndoa au mahusiano ya kimapenzi.

Kwa jumla, asilimia 52 ya wanawake Kenya wameripoti kudhulumiwa kimwili huku waliodhulumiwa kingono wakiwa asilimia 43.Suala la ukatili wa kinyumbani unaofahamika pia kama ukatili unaotekelezwa na mpenzi wa karibu, haliathiri Kenya pekee bali ni kero kuu ulimwenguni kote kwa jumla.

Karibu thuluthi moja ya wanawake kote duniani wamepitia ukatili wa kimwili au kingono maishani mwao kutoka kwa mpenzi wa karibu jinsi inavyoashiriwa na ripoti mpya ya Shirika la Afya Duniani (WHO).

Kulingana na WHO, takriban asilimia 27 ya wanawake wenye umri kati ya 15 na 49 waliowahi kuwa katika mahusiano wa kimapenzi, wamepitia aina moja au nyingine ya ukatili wa kimwili au kingono kutoka kwa mpenzi wa karibu.

Karibu nusu ya vifo vyote vya wanawake kote duniani hutekelezwa na wapenzi wao wa karibu, kulingana na takwimu.Kando na matatizo ya kiakili, janga la Covid-19 limetajwa kama kiini kikuu kulingana na ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu Dhuluma dhidi ya Wanawake 2021.

Kenya ni moja kati ya mataifa yaliyoahidi kukomesha aina zote za dhuluma za kijinsia kufikia 2030 ili kufanikisha Malengo ya Kustawisha Maendeleo (SDGs).Serikali imejitolea kufanikisha haya kupitia mpango wa kuangazia dhuluma za kijinsia uliozinduliwa na Rais Uhuru Kenyatta mnamo Juni, mwaka huu.

Ili kuzima jinamizi hili ni sharti mikakati kabambe ibuniwe inayojumuisha sekta zote katika jamii, kuambatana na katiba ya Kenya inayomhakikishia kila mwananchi ulinzi dhidi ya dhuluma za [email protected]

You can share this post!

Shahbal apuuza ‘jeshi’ la Nassir

City Stars, Homeboys na Bandari zawika ligi ikianza kushika...

T L