NA MHARIRI
KAMATI ya Bunge inayohusika na masuala ya Haki na Katiba (JLAC) hatimaye imempiga msasa Askofu Dkt David Oginde.
Askofu huyo mstaafu wa Kanisa la Christ Is The Answer Ministries (CITAM), amependekezwa achukue uongozi wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC).
Mwenyekiti aliyeondoka pia alikuwa Askofu Mstaafu wa Kanisa la Kianglikana (ACK), Dkt Eliud Wabukala.
Alipokuwa akiondoka afisini baada ya miaka sita, Dkt Wabukala alikiri kwamba hakuwa ametimiza yote aliyotarajiwa na Wakenya. Kati ya aliyochangia yeye kutokamilisha malengo ya EACC ni yale ambayo Dkt Oginde anapanga kuyashughulikia pindi atakapoingia kazini. Kwenye mahojiano ya kupigwa msasa, Dkt Oginde alitoa pendekezo ambalo linastahili kuwekwa kwenye sheria mara moja.
Anapendekeza sheria kuhusu kesi za ufisadi irekebishwe ili iwe kama ile ya kesi ya uchaguzi wa magavana hadi MCA. Anaamini kwamba kukiwa na sheria ya kuweka muda kama huo, haswa kwa kesi kama vile, Anglo Leasing, KEMSA, nchi itapiga hatua kubwa katika vita dhidi ya ufisadi. Jambo kama hili linafanyika katika mataifa kama vile Singapore ambapo vita dhidi ya ufisadi hunapewa kipaumbele.
Aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga aliweka kanuni katika Mahakama ya Juu kwamba kesi ya uchaguzi wa Magavana hadi MCA zisikizwe na kuamuliwa ndani ya miezi sita. Katiba iliweka muda wa kusikizwa na kuamuliwa kwa kesi ya uchaguzi wa urais kuwa siku 14.
Dkt Oginde ametajwa kuwa anayeheshimika nchini na ng’ambo kutokana na sifa yake ya kuwa mtu mwenye maadili. Kwamba amefanya kila awezalo kuendeleza maadili na utawala bora katika jamii. Kama bunge litampitisha, basi halina budi kuzingatia ushauri wake kuhusu muda wa kusikizwa na kuamua kesi kuhusu ufisadi.
Ripoti mbalimbali za kimataifa zinaonyesha jinsi Kenya imeathiriwa na jinamizi la ufisadi. Itakuwa mzaha kwa nchi kuweka kipaumbele kesi za uchaguzi, na kuacha kesi kuhusu ufisadi kujikokota kwa hata zaidi ya miaka kumi.
Kuchelewesha kesi za ufisadi huwa na athari nyingi. Mara kwa mara kesi hizi hupotea tu kutokana na baadhi ya mashaidi kufa wakiwa wanasubiri kueleza mahakama kuhusu wanachojua.
Ni muhimu pia kuzingatia pendekezo kwamba taasisi na afisi zinazohusika kwenye uchunguzi wa kesi za ufisadi, zifanye kazi kwa pamoja.
Kwa mfano badala ya afisa wa DCI kufanya uchunguzi peke yake ndipo awasilishe faili kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), mbona wasishirikiane na hadi afisa wa EACC?
Wanaposhirikiana na kuwasilisha kesi kortini, afisi zote tatu zitakuwa zimekubaliana kwamba upo ushahidi wa kutosha wa kushinda kesi. Bila hivyo, nchi itateua kila siku wasimamizi wa EACC bila ya kuwa na manufaa kwa mwananchi.