NA MHARIRI
HATUA ya vigogo serikalini kuelekezea ghadhabu zao wanahabari na vyombo vya habari katika juhudi za kuzima maandamano yanayoongozwa na kinara wa Azimio Raila Odinga, inafaa kukemewa vikali.
Inasikitisha kwamba vitisho hivi vinatolewa na viongozi wa ngazi ya juu serikalini walioapa kulinda Katiba na wanaofaa kuwa katika mstari wa mbele kukemea maafisa wa polisi wanaohangaisha wanahabari.
Baadhi ya wakuu serikalini jana walinukuliwa wakisema kuwa maandamano ya Azimio yanayofanyika kila Jumatatu na Alhamisi, ni ya ‘kishetani’. Labda hii ndiyo sababu ya maafisa wa polisi kulenga wanahabari kwa kupeperusha maandamano ya kishetani! Kujaribu kunyamazisha wanahabari ni kukiuka Katiba ambayo imeruhusu uhuru wa vyombo vya habari na kuwezesha Wakenya kupata habari.
Kifungu cha 34 (2) cha Katiba kinasema kuwa serikali haifai kutatiza mtu yeyote anayehusika na upeperushaji, utengenezaji au uzambazaji wa habari. Katiba pia imepiga marufuku kuadhibu yeyote anayetoa maoni yake kupitia vyombo vya habari. Nchi zinazozingatia uhuru wa vyombo vya habari zinakua kidemokrasia na kustawi kiuchumi. Hivyo, kujaribu kunyonga vyombo vya habari ni kunyonga demokrasia na ustawi wa kiuchumi.
Ripoti kwamba serikali inalenga kufunga intaneti na kuzuia baadhi ya vyombo vya habari kupeperusha maandamano ya leo mbashara ni ishara kwamba nchi inaelekea pabaya. Ni kweli kwamba baadhi ya waandamanaji wamekuwa wakizua rabsha kwa kupambana na maafisa wa polisi na kuharibu mali. Vilevile, ni kweli kwamba si jukumu la vyombo vya habari kulinda waandamanaji na kuhakikisha kuwa wanaandamana kwa amani.
Jukumu la vyombo vya habari ni kufahamisha umma yanayotokea. Hivyo, vyombo vya habari au wanahabari hawafai kulaumiwa kutokana na uharibifu huo. Ni jukumu la maafisa wa usalama kuhakikisha kwamba wanahabari wanaofuatilia maandamano wanakuwa salama. Wanahabari si maadui wa serikali bali wanatekeleza jukumu lao la kufahamisha umma kuhusu yanayoendelea nchini.
Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), Inspekta Jenerali wa Polisi (IG) na Mamlaka ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (Ipoa) hawana budi kuchunguza na kuwashtaki maafisa wa polisi ambao wamekuwa wakitumia nguvu kupita kiasi dhidi ya wanahabari. Maafisa wa polisi wanastahili kudumisha kaulimbiu yao ya “Utumishi kwa Wote” bila upendeleo.
Serikali pia inafaa kuzingatia wito uliotolewa jana na vyama vya wanahabari kutaka wanahabari waliojeruhiwa na maafisa wa polisi katika maandamano walipwe fidia. Hatua hiyo itakuwa ishara kwamba serikali haiungi mkono maafisa wa polisi ambao wamekuwa wakishambulia wanahabari na iko tayari kuwachukulia hatua kali wahusika.