• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Amerika yapepeta Mexico kwenye fainali ya Concacaf Nations League

Amerika yapepeta Mexico kwenye fainali ya Concacaf Nations League

Na MASHIRIKA

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

KIUNGO wa Chelsea, Christian Pulisic, alifunga bao katika dakika za mwisho na kusaidia timu yake ya Amerika kupepeta Mexico 3-2 kwenye fainali ya Concacaf Nations League.

Amerika walitoka nyuma mara mbili na kulazimisha mshindi wa mechi hiyo kuamuliwa katika muda wa ziada.

Pulisic, 22, aliwafungia Amerika bao la ushindi kupitia penalti iliyotolewa baada ya refa kurejelea teknolojia ya VAR kwa muda mrefu. Tukio hilo lilimkera kocha Gerardo Martino wa Mexico ambaye hatimaye alionyeshwa kadi nyekundu kwa kumchemkia refa John Pitti kwa maamuzi ya kuwapa Amerika penalti.

Kipa Ethan Horvath wa Mexico aliyetokea benchi katika kipindi cha pili alipangua mkwaju mwingine wa penalti ambayo Amerika walipewa katika mchuano huo uliopigiwa ugani Denver Empower Field.

Kipute cha Nations League kilichoanzishwa mahususi kwa vikosi vya Amerika Kaskazini, Amerika ya Kati na Caribbean husakatwa kila baada ya miaka miwili.

Mexico walitangulia kufunga kupitia Jesus Corona kabla ya Giovanni Reyna kusawazisha mambo. Ingawa Diego Lainez aliwarejesha Mexico uongozini, juhudi zake zilifutwa na Weston McKennie kabla ya Pulisic kufunga bao la ushindi.

Pulisic alielekea moja kwa moja kujumuika na kikosi cha Amerika baada ya kuongoza Chelsea kutia kapuni taji la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Mei 29, 2021.Amerika wamepangiwa kucheza na Costa Rica katika mchuano ujao wa kirafiki mnamo Juni 9, 2021.

You can share this post!

Gozi la Community Shield kati ya Man-City na Leicester...

KBC kupeperusha Safari Rally, imesaini kandarasi na WRC ya...