• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Kocha Ronald Koeman wa Barcelona asema amechoka kujitetea kutokana na matokeo duni

Kocha Ronald Koeman wa Barcelona asema amechoka kujitetea kutokana na matokeo duni

Na MASHIRIKA

KOCHA Ronald Koeman ambaye anakabiliwa na presha tele ya kupigwa kalamu na Barcelona amesema “amechoka” na matukio ya kujitetea mara kwa mara.

Kwa mujibu wa ripoti, mkufunzi huyo raia wa Uholanzi yuko pua na mdomo kutimuliwa na Barcelona baada ya miamba hao wa Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) kupoteza michuano miwili ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu huu.

Anapojiandaa kuongoza kikosi chake kumenyana na mabingwa watetezi wa La Liga, Atletico Madrid, mnamo Oktoba 2, 2021, Koeman amesema kwamba mustakabali wake uwanjani Camp Nou haujulikani ila ana uhakika kwamba “umening’inizwa padogo” baada ya vichapo kutoka kwa Bayern Munich na Benfica kwenye hatua ya makundi ya UEFA.

“Hakuna yeyote ambaye amezungumza nami. Rais wa klabu, Joan Laporta, alikuwa hapa lakini sijafaulu kumuona kwa sababu tulikuwa tukijiandaa kwa mechi ijayo dhidi ya Atletico,” akatanguliza Koeman.

“Ningali hapa lakini nina macho na masikio ya kuchuja mengi yanayoendelea na kusikia. Hata hivyo, nimechoka kujitetea mara kwa mara kikosi kinapofanya vibaya. Haina haja kabisa. Leo si wakati mzuri ila naamini ipo siku ambapo nitazungumza kwa kina kuhusu mambo yanayosibu Barcelona kwa sasa,” akasema Koeman.

Ingawa hivyo, kocha huyo wa zamani wa Everton na timu ya taifa ya Uholanzi alikataa kujibu maswali ya jinsi anavyohusiana na Laporta na badala yake akasisitiza: “Ningali hapa.”

Uhusiano kati ya Laporta na Koeman ulianza kuingia baridi tangu Machi 2021 kinara huyo aliporejea kudhibiti usukani wa urais kambini mwa Barcelona.

Barcelona wamekuwa wakikabiliana na panda-shuka tele tangu waagane na supastaa raia wa Argentina, Lionel Messi aliyeyoyomea Ufaransa kuvalia jezi za Paris Saint-Germain (PSG) mwanzoni mwa msimu huu wa 2021-22.

Baada ya kupigwa 3-0 na Bayern katika mchuano wa kwanza wa UEFA msimu huu ugani Camp Nou, Barcelona walipokezwa kichapo sawa na hicho na Benfica mnamo Septemba 29 nchini Ureno.

Kufikia sasa, wanashikilia nafasi ya sita kwenye msimamo wa jedwali la La Liga huku pengo la alama tano likitamalaki kati yao na viongozi Real Madrid. Barcelona wamesajili sare tatu kutokana na mechi sita zilizopita za La Liga.

Kulingana na magazeti mengi nchini Uhispania, ni suala la muda tu kabla ya Koeman kupigwa kalamu na Barcelona waliojivunia huduma zake akiwa mchezaji mnamo 1992 waliponyanyua taji la European Cup.

  • Tags

You can share this post!

Wachezaji wa Brighton na Southampton katika kikosi cha Mali...

SHAIRI: Msichana ni muhimu, heri kumsaidia