NA MASHIRIKA
BUENOS AIRES, Argentina
WAHUDUMU wanane wa afya watafikishwa mahakamani kwa madai ya utelekezaji katika kifo cha mwanasoka nyota Diego Maradona kutoka Argentina.
Jaji mmoja ameamrisha mashtaka ya mauaji yafanywe baada ya jopo la madaktari kugundua kuwa matibabu ya Maradona yalijaa “mapungufu na ukiukaji wa utaratibu”.
Maradona aliaga dunia Novemba 2020 kutokana na mshtuko wa moyo jijini Buenos Aires akiwa na umri wa miaka 60.
Alikuwa akiendelea kupata afueni nyumbani baada ya kufanyiwa upasuaji kuondoa damu iliyoganda ubongoni mapema mwezi huo.
Siku chache baada ya kifo hicho, waendesha mashtaka nchini Argentina walianzisha uchunguzi dhidi ya madaktari na wauguzi waliohusika katika kumtunza.
Mwaka jana, jopo la wataalamu 20 lililoteuliwa kuchunguza maafisa hao wa afya liliwapata na makosa.
Maafisa hao wamekana kuhusika kivyovyote na kifo cha Maradona.