• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Nyumba Yangu: Wanariadha kunufaika kupitia ushirikiano wa AK na HFC Group

Nyumba Yangu: Wanariadha kunufaika kupitia ushirikiano wa AK na HFC Group

AYUMBA AYODI na GEOFFREY ANENE

Maelfu ya wanariadha wa Kenya wanatarajiwa kunufaika mpango wa nyumba za bei nafuu kati ya Shirikisho la Riadha Kenya na Benki ya kutoa mikopo ya ujenzi na ununuzi wa nyumba nchini (HFC Group).

Pande hizo zilisaini mapatano jijini Nairobi hapo Mei 30.

Ushirikiano huo utawezesha wanariadha kuweka akiba ili kuwawezesha kumiliki nyumba kupitia mpango wa serikali wa nyumba za bei nafuu.

Kile wanariadha watahitajika kufanya ni kufungua akaunti ya “Nyumba Yangu” katika benki hiyo ambapo wataweka asili ya chini ya 12.5 ili kumiliki nyumba.

Waziri wa Michezo Ababu Namwamba aliongoza shughuli ya kusaini maelewano hayo kati ya rais wa AK Jack Tuwei na Afisa Mkuu Mtendaji wa HFC Group, Robert Kibaara, katika hoteli ya Weston, Nairobi.

Kibaara alifichua kuwa wazo hilo lilimjia alipokutana na Tuwei siku moja kwenye makao makuu ya riadha nchini Riadha House kujadiliana kuhusu fursa ya wanariadha na familia ya AK kuwa na nyumba zao.

“Inachukua bidii ya mchwa wanariadha wetu kuwa mabingwa wa dunia na si kwa bahati kwa hivyo ni jukumu letu kama taifa kuwasaidia kuwekeza katika vitu vya maana,” alisema Kibaara, akitaja kuwa kumiliki nyumba ni kitu cha maana sana.

Namwamba alitaja ushirikiano huo kuwa wa busara na utakaofaidi wanariadha na familia ya AK na kuwataka waukumbatie.

“Haikubaliki kuwa tunaposherehekea miaka 60 tangu tupate uhuru, bado tunaendelea kushuhudia mitaa ya mabanda ikiongezeka. Wakazi wengi wa mijini wanaishi katika hali ya kusikitisha bila ya kusahau wanamichezo wetu,” alisema Namwamba.

Mabingwa wa Jumuiya ya Madola Mary Moraa (mbio za mita 800) na Beatrice Chebet (5,000m), mshikilizi wa rekodi ya dunia mbio za 3,000m kuruka viunzi na maji Beatrice Chepkoech na watimkaji wa mbio fupi Wiseman Were na Dan Kiviasi walihudhuria hafla ya kusaini mapatano hayo.

Majagina Cathrine Ndereba, John Ngugi na Sally Barsosio pamoja na bingwa wa Olimpiki mbio za 800m mwaka 2008 Wilfred Bungei, pia walihudhuria hafla hiyo.

  • Tags

You can share this post!

Akaunti za M-Pesa za Pasta Ezekiel Odero zafunguliwa...

Amerika yaadhibu spika wa Uganda kwa kupitisha sheria...

T L