• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Vissel Kobe inayoajiri Mkenya Masika iko mguu mmoja nje ya Kombe la Levain, imepigwa Jumapili

Vissel Kobe inayoajiri Mkenya Masika iko mguu mmoja nje ya Kombe la Levain, imepigwa Jumapili

Na GEOFFREY ANENE

VISSEL Kobe anayochezea Ayub Masika inakodolea macho kubanduliwa kwenye kipute cha Levain Cup baada ya kupoteza mechi ya mkondo wa kwanza ya robo-fainali 2-1 dhidi ya wageni Urawa Red Diamonds ugani Noevir, Jumapili.

Vissel ilianza vyema mchuano huo mbele ya mashabiki 4,720. Mshambuliaji wa Brazil, Douglas aliweka wenyeji kifua mbele dakika ya tatu kutokana na kona.

Dakika nne baadaye, Masika alinyimwa na beki wa Urawa Reds and taifa la Australia, Thomas Deng ambaye ni mzawa wa Kenya, nafasi ya kuimarisha uongozi huo.

Vissel ilitumia pasi ndefu, lakini mbinu hiyo haikuwasaidia sana kwani safu ya ulinzi ya Urawa iliondosha mipira hiyo.Masika alikosa fursa nyingine nzuri dakika ya 17 alipopokea pasi safi kutoka kwa kiungo stadi wa Uhispania na Barcelona, Andres Iniesta.

Sekunde chache baadaye, Hotaru Yamaguchi alipoteza nafasi nzuri baada ya kupokea pasi kutoka kwa Iniesta.

Urawa ilianza kuwekea presha wenyeji wao baada ya mapumziko ya kunywa maji dakika ya 23. Walifanya shambulizi baada ya jingine, ingawa waliponea kujipata mabao mawili chini dakika ya 39 wakati Masika alikosa lango kipa alipotema mpira.

Atsushi Ito alisawazisha 1-1 alipokamilisha pasi ndefu kutoka kwa Takahiro Sekine kabla tu ya dakika 45 za kwanza kukatika.Krosi ya mapema katika kipindi cha pili kutoka kwa Ryo Hatsuse iliyoelekezwa langoni mwa Urawa kutoka kwa Masika ilinyakwa kwa urahisi na kipa Shusaku Nishikawa.

Nafasi nyingine ya Vissel ilipotea dakika ya 55 baada ya beki mmoja kupangua shambulizi lililofanywa na Iniesta akishirikiana na Douglas.Nishikawa aliondosha hatari nyingine kutoka kwa Masika sekunde chache baadaye.

Vijana wa kocha Atsuhiro Miura walijaribu kila mbinu kupata bao la kuwarejesha juu, lakini bila mafanikio.Vissel ilifanya mabadiliko mawili dakika ya 61 ikiwaingiza Mbrazil Lincoln na Sasaki katika nafasi ya Douglas na Masika, mtawalia.

Hata hivyo, Urawa ndio ilipata tabasamu la mwisho baada ya Shinzo Koroki kuifungia bao la ushindi dakika ya 70 beki Ryo Kikuchi alipoteleza akiwa amepigiwa pasi ya nyuma na mwenzake Yamaguchi.

Katika michuano mingine ya robo-fainali Jumapili, Hokkaido Consadole Sapporo na Yokohama F. Marinos zlitoka 1-1 mjini Sapporo, huku Kashima Antlers ikitwanga wageni Shimizu S-Pulse 2-1. Shonan Bellmare iliduwaza mabingwa watetezi FC Tokyo 1-0 Jumamosi.

Kashima tayari iko katika nusu-fainali baada ya kuchabanga Shimizu 1-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza 1-0 Juni 2. Mechi za marudiano za timu hizo nyingine ni Juni 13.

You can share this post!

Mkenya Mudibo achaguliwa naibu rais wa tenisi ya mezani...

Utangamano wa kitaifa ni moja ya malengo muhimu ya elimu,...