Na GEOFFREY ANENE
ZAIDI ya wachezaji 280 wa gofu watakusanyika katika uwanja wa klabu ya gofu ya Ruiru katika kaunti ya Kiambu kuwania ubingwa wa mashindano ya Legendary hapo Septemba 2.
Kwenye mashindano hayo yanayodhaminiwa na kampuni za Edlon Group, Corporate Masters, Bransons Kitchen, Grandstart na AfrInsight Consulting, wachezaji watawania pointi katika mashimo 18.
Tabitha Kiragu, ambaye aliibuka mshindi wa makala ya kwanza ya mashindano ya IPF ugani humo wikendi iliyopita, pamoja na Emmanuel Wachira, Mary Wambui na David Kibui ni baadhi ya wachezaji wanaopigiwa upatu kung’aa.
“Nasubiri kwa hamu kuendeleza nilikoachia wikendi iliyopita. Nililemea zaidi ya wachezaji 190. Hata hivyo, najua kibarua kitakuwa kikali kwa sababu gofu ya Legendary imevutia wanagofu wazuri kutoka kote nchini. Naamini uzoefu wangu na hali yangu nzuri ya mchezo wakati huu zitanisaidia kuibuka na ushindi,” akasema Kiragu, Jumatano.
Nahodha wa klabu ya Ruiru, Jessy Ndegwa amesema wanafurahia kuwa wenyeji wa baadhi ya majina makubwa katika mchezo huo nchini Kenya.
Gofu ya Legendary ni sehemu ya msururu wa shughuli klabu ya Ruiru imekuwa ikifanya mwaka 2023 ambapo benki ya KCB ni moja ya mashirika yamefanyia mashindano yake katika kituo hicho kinachoadhimisha miaka 100.