• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Wanaraga wa Machine wazidia nguvu Egerton Wasps

Wanaraga wa Machine wazidia nguvu Egerton Wasps

Na GEOFFREY ANENE

TIMU ya raga ya Chuo Kikuu cha Nairobi almaarufu Mean Machine imelipua Egerton Wasps ya Chuo Kikuu cha Egerton 37-0 jijini Nairobi mnamo Jumamosi na kuingia nusu-fainali ya kuwania tiketi ya kupandishwa daraja ya kushiriki Ligi Kuu.

Machine, ambayo ilitemwa kutoka Ligi Kuu (Kenya Cup) misimu kadhaa iliyopita, imetumia Chuo Kikuu cha Masinde Muliro (MMUST) onyo kali kwa kuzamisha Wasps kupitia miguso ya Grevis Onyino, Lawrence Ndung’u, Marvin Karungi na Bruce Odhiambo. Festus Shiasi alichangia penalti moja na mkwaju naye Trevor Asina alifunga penalti nne.

MMUST ilifuzu moja kwa moja kushiriki nusu-fainali ilipomaliza Ligi ya Daraja ya Pili katika nafasi ya pili katika msimu wa kawaida 2019-2020.

Itaaalika Machine mjini Kakamega kwa mechi ya nusu-fainali hapo Februari 13.

Mechi kati ya Machine na Wasps ilikuwa mechi ya kwanza ya raga kufanyika Kenya katika kipindi cha miezi 11 baada ya mkurupuko wa virusi vya corona kukatika shughuli ya msimu uliopita kwa ghafla Machi 2020. Machine ilifurahia uongozi wa alama 19-0 wakati wa mapumziko na haikuwapa Wasps nafasi ya kurudi kwenye mechi hiyo.

Matokeo hayo yanamaanisha kuwa Machine iko pazuri kurejea Kenya Cup muradi ifaulu kunyamazisha MMUST uwanjani mwao Kakamega.

Mshindi wa nusu-fainali hiyo atajikatia tiketi ya kujiunga na Kabras Sugar, KCB, Homeboyz, Impala Saracens, Mwamba, Menengai Oilers, Nakuru, Blak Blad, Kenya Harlequin na Nondescripts kwenye Ligi Kuu. Itakuwa mara ya kwanza kabisa MMUST kushiriki Kenya Cup ikikung’uta mabingwa wa mwaka 1977, 1989 na 1990 Machine.

Bingwa wa nusu-fainali nyingine kati ya Leos ya Chuo Kikuu cha Strathmore na Northern Suburbs pia ataingia Kenya Cup msimu ujao wa 2021. Leos ilishinda msimu wa kawaida wa ligi hiyo ya daraja ya pili kwa hivyo itakuwa mwenyeji wa Suburbs katika uwanja wake wa Madaraka.

You can share this post!

Kambi ya Olunga imani tele ikiendea Ulsan Hyundai

Rotich adhihirishia Kinyamal nani mfalme wa mbio za mita 800