Na GEOFFREY ANENE
ZAIDI ya waogeleaji 200 wamethibitisha kushiriki mashindano ya kuogelea ya Shirikisho la Uogeleaji Kenya (KSF) tawi la Kiambu katika shule ya kimataifa ya Crawford inayopatikana eneo la Tatu City, Kiambu.
Mashindano haya ni ya 12 na mwisho msimu huu wa 2022-2023 ya tawi hilo.
Waogeleaji waliotoa ithibati ya kushiriki wanatoka katika timu 14 kutoka kaunti ya Nairobi, Murang’a na Kiambu.
Shule nne za kimataifa zilizoingia mashindano haya ni wenyeji Crawford pamoja na Woodcreek, Aga Khan Academy na Regis.
Klabu zitakazoshiriki ni Super Marlins, Condor, Sea Horses na Pamoja Arts & Multi Sports International.
Shule ya msingi ya kibinafsi ya ACK Memorial kutoka Thika na shule ya msingi ya umma ya Mugumo-Ini zitashiriki mashindano ya KSF-Kiambu kwa mara ya kwanza kabisa.
Gavana wa KSF, Stanley Kaberu amefichua kuwa Mugumo-Ini itashiriki mashindano chini ya mpango wa majukumu ya shirika la kijamii. KSF-Kiambu itawapunguzia ada ya kushiriki.
“Juhudu hizi ni za kuinua talanta ya uogeleaji kutoka familia zisizojiweza kifedha,” akasema.
Afisa wa uhusiano wema wa KSF-Kiambu Nesmas Mbati ameeleza kuwa washiriki watakaotimiza muda ya kufuzu wataingia mashindano ya kiwango cha kwanza mnamo Agosti 26-27 katika akademia ya Mpesa Foundation, Thika.
KSF-Kiambu pia inapanga hafla ya kutuza waogeleaji na kuwa na mkutano wake wa kila mwaka mwezi wa Julai.