• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:15 AM
West Brom washuka ngazi kutoka EPL baada ya kupepetwa na Arsenal

West Brom washuka ngazi kutoka EPL baada ya kupepetwa na Arsenal

Na MASHIRIKA

WEST Bromwich Albion waliteremshwa ngazi kutoka Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) hadi Ligi ya Daraja la Kwanza (Championship) kwa mara ya tano baada ya kupokezwa kichapo cha 3-1 kutoka kwa Arsenal mnamo Jumapili ugani Emirates.

Ushindi huo wa Arsenal uliwadumisha West Brom almaarufu ‘The Baggies’ katika nafasi ya 19 kwa alama 26 huku pengo la alama 10 likiwatenganisha na Burnley wanaokamata nafasi ya 17. Zimesalia mechi tatu pekee kabla ya kampeni za EPL msimu huu kutamatika rasmi.

Emile Smith Rowe alifunguliwa Arsenal karamu ya mabao katika dakika ya 29 baada ya kushirikiana na Bukayo Saka aliyechangia pia goli la pili ambalo Arsenal walifungiwa na fowadi Nicolas Pepe katika dakika ya 35.

Ingawa Matheus Pereira alipania kurejesha waajiri wake mchezoni alipofunga bao katika dakika ya 67, juhudi chombo cha West Brom kilizamishwa kabisa na kiungo Willian Borges aliyecheka na nyavu mwishoni mwa kipindi cha pili.

Arsenal waliodenguliwa na Villarreal kwenye nusu-fainali ya Europa League mnamo Mei 6, 2021, wanashikilia nafasi ya tisa jedwalini kwa alama 52.

Hii ni mara ya kwanza kwa kocha Sam Allardyce wa West Brom kushushwa daraja kwenye EPL akiwa kocha.

Mkufunzi huyo mwenye umri wa miaka 66 aliaminiwa fursa ya kuwa mrithi wa kocha Slaven Bilic aliyetimuliwa na West Brom mnamo Disemba 2020 kikosi hicho kikishikilia bado nafasi ya 19 kwenye msimamo wa jedwali.

Allardyce aliwahi kufaulu kuwaongoza Blackburn Rovers, Sunderland na Crystal Palace kusalia kwenye kipute cha EPL baada ya kupokezwa mikoba wakati vikosi hivyo vikiwa katika hatari ya kuteremshwa ngazi ligini.

Lakini juhudi za kuokoa chombo cha West Brom mara hii ziliambulia pakavu huku kikosi hicho kikifanikiwa kusajili ushindi mara nne pekee kutokana na mechi 22 zilizosimamiwa na Allardyce ambaye pia amewahi kudhibiti mikoba ya timu ya taifa ya Uingereza.

Arsenal kwa sasa wanajiandaa kupepetana na Chelsea ligini mnamo Mei 12 ugani Stamford Bridge huku West Brom wakiwaalika Liverpool uwanjani The Hawthorns siku nne baadaye.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Juventus katika hatari ya kukosa UEFA msimu ujao

Everton wakomoa West Ham ligini na kuweka hai matumaini ya...