NA CECIL ODONGO
WANAUME wanene wanahangaishwa na maradhi zaidi kuliko wanawake, Utafiti umebaini.
Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha York Canada wamegundua kuwa kuna tofauti za kibayolojia kati ya seli zinazojenga mishipa ya damu kwenye mwanaume na mwanamke.
Tofauti kwenye seli hizo ndizo huchangia wanaume wenye unene kuandamwa na maradhi sugu.
Kati ya maradhi sugu ambayo wanaume wanene wapo katika hatari ya kuyapata ni ugonjwa wa moyo, kisukari, shinikizo la damu, kiharusi na maradhi haya huweza kusababisha kifo.
Utafiti huo ulibaini kuwa mwanamke anapokuwa mnene, mishipa mipya ya damu hujitokeza na husambaza mafuta kinyume na mwanaume ambapo mishipa husalia ile ile kisha mara nyingi mafuta huganda katika sehemu moja.
Pia, watafiti hao walibaini kuwa mishipa ya damu huwa haiongezeki kwa mwanaume mnene na mara nyingi ile iliyoko hutanuka tu kutokana na wingi wa mafuta. Hii ni kinyume kwa mwanamke ambapo mishipa mipya hujengeka mara kwa mara na kusafisha mafuta kwenye njia ya damu.
Ili kuepekuna na mafuta mengi mwilini, wanaume hushauriwa kufanya mazoezi mara kwa mara na pia kutokula vyakula ambavyo huongeza mafuta mwilini.
Wakati wa mazoezi, mwili huhitaji nguvu za ziada na hilo husaidia kuchoma mafuta kisha kuyaelekeza kwenye damu ndipo misuli hupata nguvu zinazohitajika kuendelea na mazoezi.
Vile vile, mwanaume hushauriwa kula vyakula ambavyo vinasaidia mwili kupunguza unene. Vyakula hivyo, ni kama maharagwe, mboga na nafaka mbalimbali.
Kuzuia unene kupita kiasi, mwanaume mwenye unene hutakiwa kula vyakula vyenye madini yote.