Na RICHARD MUNGUTI
AFISA wa polisi ameshtakiwa kushindwa kulipa pombe aliyobugia na sigara alizofuta.
Perminus Nderitu alikabiliwa na shtaka la kubugia mfinyo na kuvuta sigara za bei ghali akijua hakuwa na pesa za kutosha kuzilipia. Mahakama ilifahamishwa Nderitu alipokea vinywaji hivyo katika kituo cha kuuza ya Petroli cha Rubis,Westlands Nairobi.
Pombe na Sigara alizotumia zilikuwa za thamani ya Sh1, 860. Alishtakiwa kwa kupata bidhaa akidai alikuwa na uwezo wa kuzilipia. Hakimu mwandamizi Derrick Kutto alielezwa mshtakiwa alikuwa na mtu mwingine ambaye pia aliagiza pombe ya kubeba kuishughulikia akiwa njiani.
Nderitu alikanusha shtaka na kuomba Bw Kutto amwachilie kwa dhamana. Aliachiliwa kwa dhamana ya pesa tasilimu Sh10,000 Kesi itasikizwa Aprili 7,2022.