NA CHARLES WASONGA
MAAFISA wa polisi wamezingira boma la kibinafsi la aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i katika mtaa wa Karen, Nairobi wakipanga kumkamata.
Mawakili wake wakiongozwa na Danstan Omari wanasema hawafahamu ni kwa nini maafisa hao wanataka kumkamata Dkt Matiang’i majira ya usiku.
“Tunashuku kuwa maafisa hao wanataka kumwekelea makosa kisha kumshtaki. Hii ndiyo maana sisi kama mawakili wake hatutatoka hapa mpaka tuambiwe ni kwa nini polisi wanataka kumkamata Matiang’i,” akasema, Jumatano usiku.
“Wakati huu, kile ambacho tungetaka kuwaambia Wakenya ni kwamba maisha ya Dkt Matiang’i yamo hatarini,” Bw Omari akawaambia wanahabari.
Kiongozi wa upinzani Raila Odinga pia amefika nyumbani kwa Dkt Matiang’i baada ya kufahamishwa kwamba maafika wa polisi wamefika hapo wakilenga kumkamata.
“Ikiwa Matiang’i amefanya kosa lolote, yeye ni Mkenya aagizwe kufika kwa polisi na kuandikisha taarifa. Polisi hawafai kuenda katika makazi yake majira ya usiku wakitaka kumkamata? Huu ni uhalifu. Huu sio ustaarabu. Nimekuwa nikisema kwamba hii ni serikali isiyo halali,” akasema Bw Odinga aliyeonekana mwenye hasira.
Kiongozi huyo wa Azimio la Umoja-One Kenya aliulaani utawala wa Rais William Ruto kwa kutumia polisi kuvunja sheria.
Wakili mwingine, Sam Nyaberi amesema zaidi ya mawakili 200 wamemzingira Dkt Matiang’i ndani ya chumba ambako amejifungia na watakaa naye usiku kucha.