Na JOHN KIMWERE
INGAWA bado hajapata umaarufu mkubwa katika jukwaa la muziki wa burudani ameibuka kati ya wasanii wanaozidi kujituma mithili uya mchwa kwenye jitihada za kukuza kipaji chao.
Enock Wilson Teyie maarufu Rusty Gee amekuwa akipigana na matumizi ya mihadarati pia visa vya ubakaji kupitia muziki tangia mwaka 2015. Ndani ya miaka michache iliyopita kupitia serikali ya Kaunti ya Vihiga amekuwa katika mstari wa kwanza kwenye juhudi za kutambua wasanii wanaokuja eneo hilo.
Tamasha
Mapema mwaka huu serikali ya Kaunti hiyo kupitia wizara ya vijana na michezo waliandaa tamasha la sanaa kwa jina Vihiga Extravanza. ”Kupitia tamasha hilo tulipata wasanii watatu Micky Eric na Kevoh Ali (wanaume) na mwana dada mmoja Jaycy,” anasema na kuongeza kuwa ni furaha kwake kuona kwamba kupitia jitihada zake serikali hiyo imeanza kukumbatia sekta ya burundani eneo hilo.
Msanii huyu anasema kuwa serikali iligharamia ada ya kurekodi nyimbo tatu kwa wasanii hao. Gavana wa Kaunti hiyo, Daktari Wilber Ottichilo anasema watakuwa wakiandaa tamasha kama hiyo kila mwaka nia kuu ikiwa kutoa nafasi kwa wasanii chipukizi kutambua vipaji vyao.
Rusty Gee anashukuru Waziri wa wizara hiyo, Felistus Okumu na kamati yake nzima ikiwamo Philip Gavuna na Humprey Kisia kati ya wengine kwa kukubali kuandaa tamasha hiyo.
Sugarmummy
”Binafsi ningependa kutoa wito kwa serikali za Kaunti zingine kuiga mfano huo kwa kuzingatia kusaidia chipukizi wengi kutambua talanta zao,” Rusty Gee alisema na kuhimiza chipukizi hao wanaokuja kuwa wasife moyo wazidi kukaza buti kwenye jitihada za kukuza talanta zao. Anadokeza kuwa sanaa ina uwezo wa kuimarisha uchumi pakubwa na pia inasadia kupigana na madawa ya kulevya, wizi na ulevi miongoni mwa vijana.
Msanii huyu (Rusty Gee) anajivunia kuachia teke kadhaa zinazozidi kutesa anga ya muziki wa burudani ambapo sasa anatamba na kibao cha Sugarmummy. Kati ya tambo zingine amechia hivi karibuni zikiwa ‘Utaomoka,’ ‘Nawabebanga,’ na ‘Naree.’
Msanii huyu mtunzi wa nyimbo za kufoka yaani Rap anasema anavutiwa na teke za injili kama ‘Hela,’ Utawala,’ – kazi yale ,wimbaji na mtunzi wa hapa nchini maarufu kama Juliani. Pia anapenda sana kuketi na kusikiza kazi yake Cannibal mwimbaji wa Mombasa kama ‘Kichwa kibovu,’ na ‘Street Hustler.”
Kwa wafuasi wake anasema watarajie kazi nyingi tu kutoka kwake. Pia anawashukuru mashabiki wake wote kwa upendo wao kwake, wanahabari wote waliompatia nafasi na kumuonyesha njia kama vile Mzazi Willy Tuva na Kazungu Mwinyi kati ya wengine.
Anashauri wasanii chipukizi wanaolenga kufanya vizuri kwamba mwanzo wanastahili kuonyesha ni dhamu na kuelewa wanacholenga katika taaluma hii fana bila kuweka katika kaburi la sahau kuwa kukumbana na pandashuka ni jambo la kawaida.