CHARLES WASONGA Na ANTHONY KITIMO
MUUNGANO wa Azimio umeteua kikosi cha wanasiasa wenye misimamo mikali kuiwakilisha kwenye meza ya mazungumzo na wawakilishi wa Kenya Kwanza kuhusu masuala yaliyosababisha mvutano kati ya mirengo hiyo.
Walioteuliwa Alhamisi wakati wa mkutano ulioongozwa na kiongozi wa Azimio Raila Odinga katika kaunti ya Machakos, ni pamoja na maseneta; Ledama Ole Kina (Narok), Edwin Sifuna (Nairobi) na Seneta wa Kitui Enoch Wambua.
Wengine ni wabunge, Amina Mnyanzi (Malindi), Millie Odhiambo (Suba Kaskazini), David Pkosing (Pokot Kusini) na Otiende Amollo (Rarieda).
Saba hao waliteuliwa wakati wa mkutano wa Kundi la Wabunge (PG) wa Azimio uliofanyika katika hoteli ya Stoni Athi, kaunti ya Machakos.
“Hawa ndio watakuwa wawakilishi wetu katika mazungumzo na upande ule mwingine. Ndio watasimama kidete kuhakikisha kuwa bei ya unga inapunguzwa, sava ya IEBC inafunguliwa na uteuzi wa makamishna wapya unaendeshwa kwa njia ya haki. Tunashikilia kuiwa mazungumzo hayo yafanyike nje ya bunge,” Bw Odinga akasema.
Lakini kuna hofu kwamba, huenda mazungumzo hayo yasifaulu kutokana na hali kwamba, wanasiasa hawa ni miongoni mwa wale wenye misimamo mikali zaidi katika kambi ya Azimio.
Kwa mfano, Mbw Ole Kina na Sifuna, pamoja na Bi Mnyanzi ni miongoni mwa viongozi wa Azimio ambao wamekuwa kwenye mstari wa mbele wakishiriki maandamano tangu Machi 20, 2023.
Siku hiyo, Bi Mnyanzi alikamatwa pamoja na kiongozi wa wachache katika bunge la kitaifa Opiyo Wandayi, mwenzake wa seneti Stewart Madzayo na Mbunge wa Kilifi Kusini Ken Chonga wakielekea jumba la KICC, Nairobi kuongoza maandamano.
Wawakilishi hao wa Azimio wanatarajiwa kuketi kwenye meza ya mazungumzo na wenzao saba kutoka mrengo wa Kenya Kwanza ambao watateuliwa Jumanne wiki ijayo.
Kiranja wa wengi katika bunge la kitaifa, Sylanus Osoro juzi alisema kuwa, viongozi hao watateuliwa katika mkutano wa kundi la wabunge (PG) wa Kenya Kwanza.
“Tutaandaa mkutano wetu wa wabunge Jumanne saa chache kabla ya bunge kurejelea vikao vyake baada ya likizo kujadili ajenda ya Kenya Kwanza. Ni katika kikao hicho ambapo wawakilishi wetu katika mazungumzo na Azimio watateuliwa,” Mbunge huyo wa Mugirango Kusini akasema Jumanne kwenye mahojiano na runinga ya Citizen.
Lakini mnamo Jumatatu, Rais Ruto alikutana na uongozi wa Kenya Kwanza katika Bunge la Kitaifa na Seneti kujadili suala hilo la mazungumzo yenye nia ya kushughulikia malalamishi yaliyoibuliwa na Azimio.
Hii ni ishara kwamba, huenda viongozi hao ni miongoni mwa wale watakaoteuliwa kuongoza mazungumzo hayo. Wao ni pamoja na; Kimani Ichung’wa (Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa), Owen Baya (Naibu Kiongozi wa Wengi Bunge la Kitaifa), Bw Osoro na Bi Naomi wake ambaye ni naibu wake.
Kutoka Seneti wale waliohudhuria mkutano huo ni; Aaron Cheruiyot (Kiongozi wa wengi) na naibu wake Tabitha Karanja, Boni Khalwale (Kiranja wa Wengi) na naibu wake Steve Lelengwe ambaye ni Seneta wa Samburu.
Miongoni mwa viongozi hawa, Bw Ichung’wa na Bw Cheruiyot wamejitokeza kama viongozi wenye misimamo mikali zaidi na ambao wamekua mstari wa mbele kupinga pendekezo la Azimio kwamba, mazungumzo hayo yafuate mkono wa Maridhiano ya Kitaifa ya 2008.
Jana, Bw Odinga na vigogo wengine walishikilia kuwa, mazungumzo hayo sharti yaendeshwe nje ya bunge, wakielezea hofu kuwa “haki haitapatikana katika bunge linalodhibitiwa na Kenya Kwanza”.
Naye Rais William Ruto jana Alhamisi alimtaka Bw Odinga kukubali mazungumzo hayo yafanywe bungeni “au asubiri hadi mwaka wa 2027 awanie urais wa mara nyingine”.
“Hatuwezi kufanya mazungumzo nje ya sheria. Hii ndio maana ninasema kuwa, tuwaruhusu wabunge, tuliowachagua, kufanya mazungunzo ndani ya bunge kusuluhisha masuala tata yaliyoyoibuliwa na wenzetu wa upinzani,” Dkt Ruto akasema katika wadi ya Kasemeni, kaunti ya Kwale, alipozindua ujenzi wa bwawa la Mwache.
“Kile ninaweza kusema ni hiki- Ikiwa mazungumzo hayatafanyika ndani ya Bunge, basi wanapaswa kusubiri uchaguzi mkuu wa 2027 ili waweze kuchaguliwa na waunde serikali,” akaeleza.