• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
JAMVI: Misimamo mikali OKA inaweza kuwafaidi au kuwabomoa 2022

JAMVI: Misimamo mikali OKA inaweza kuwafaidi au kuwabomoa 2022

Na BENSON MATHEKA

MSIMAMO mkali wa baadhi ya vinara wanaosuka muungano wa One Kenya Alliance (OKA) wa kukataa kumuunga kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga, huenda ukawa baraka kwao au ukawasukuma kwenye baridi kali zaidi ya kisiasa baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2022.

Muungano huo ambao unaendelea kusukwa, unaleta pamoja kiongozi wa chama cha Amani National Congress Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka wa chama cha Wiper, Moses Wetang’ula wa Ford Kenya na Gideon Moi wa chama cha Kanu.

Bw Mudavadi, Bw Musyoka na Bw Wetang’ula wamesimama kidete kwamba hawatamuunga Bw Odinga huku ikisemekana kuwa Bw Moi hana tatizo kumuunga waziri mkuu huyo wa zamani.

Watatu hao ambao walikuwa vinara wenza wa Bw Odinga katika uliokuwa muungano wa NASA wanasema kwamba wanaweza tu kushirikiana naye akijiunga na OKA bila masharti.

Licha ya kushauriwa na Rais Uhuru Kenyatta kumuunga Bw Odinga ili waweze kumshinda Naibu Rais William Ruto kwenye uchaguzi mkuu ujao, Bw Mudavadi na Bw Musyoka wamekaa ngumu kila mmoja akisisitiza kuwa jina lake litakuwa kwenye debe.

Kulingana na wachanganuzi wa siasa, sio siri kwamba Bw Odinga ndiye mwanasiasa maarufu zaidi kote nchini kuweza kutoa jasho Dkt Ruto na kwa kukataa kuungana naye, huenda wakapoteza nafasi ya kuwa kwenye serikali ijayo.

“Iwapo Bw Odinga atafanikiwa kuunda muungano thabiti kukabiliana na Dkt Ruto na mmoja wao apate zaidi ya asilimia 50 ya kura, vinara wa OKA watalazimika kuumia kwenye baridi ya kisiasa,” asema.

“Lakini ikiwa hakutakuwa na mshindi wa moja kwa moja wa kura ya urais kwenye uchaguzi mkuu ujao na wanawaweza kulazimisha hilo kufanyika, watakuwa katika nafasi nzuri ya kuungana na mrengo wa Bw Odinga au Dkt Ruto kwenye raundi ya pili ya uchaguzi na kuwa kwenye serikali ijayo,” asema mdadisi wa siasa Tom Maosa.

Anasema kwamba misimamo mikali pia inadhihirika ndani ya OKA na inaweza kufanya muungano huo kusambaratika hata kabla ya kuzinduliwa.

“Kuna vinara wawili ambao wanashikilia kuwa hawawezi kuunga Bw Odinga huku kila mmoja akisisitiza hawezi kumuachia mwenzake kupeperusha bendera. Hii inaweza kuchangia kuwasukuma katika baridi ya kisiasa wakikosa muafaka,” asema Maosa.

Mnamo Ijumaa, Bw Mudavadi alisema mwanasiasa yeyote anayetarajia atamuunga mkono anaota.

“Nitakuwa kwenye debe. Niko na mipango ya kuongoza Kenya kupata ustawi mkubwa wa kiuchumi,” alisema Bw Mudavadi.

Kauli yake ilijiri siku tatu baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuhimiza vinara wa OKA, kumuunga Bw Odinga kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Kulingana na mdadisi wa siasa Geff Kamwanah, vinara hao wanakabiliwa na hatari ya kujipata njia panda, iwapo Bw Odinga atafaulu kuunda muungano mpya na kuwafungia nje na kisha Rais Uhuru Kenyatta awaache kwenye mataa.

“Hali inaweza kuwa mbaya kwao iwapo Dkt Ruto atasisitiza kuwa amejipanga na hahitaji ushirika wa vigogo ambao amekuwa akidai walifanya akafukuzwa serikalini. Hii ikifanyika, watakuwa mayatima kwenye siasa za Kenya,” asema Bw Kamwanah.

“Kwa kuwa siasa za Kenya zinabadilika haraka, kuna hatari yao kujichimbia kaburi kisiasa wakikosa kwenye serikali ijayo,” aongeza mchanganuzi huyu.

Baadhi ya wadadisi wanasema misimamo ya vinara wa OKA inaweza kufanya kila mmoja wao akipigana kuokoa maisha yake ya kisiasa kivyake.

“Iwapo Bw Mudavadi atatofautiana na Bw Musyoka kuhusu anayefaa kuwa mgombea urais wa muungano wao, wanaweza kugawanyika na kulegeza msimamo mmoja aelekee kwa Dkt Ruto na mwingine kwa Bw Odinga. Hii inaweza kubadilisha mkondo wa siasa kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022,” asema Bw Richard Kakai, wakili na mdadisi wa siasa.

Kulingana na Bw Kakai, makosa ambayo wawili hao wanaweza kufanya ni kutengana na kila mmoja kugombea kivyake.

“Kutengana kwao, ambao kunaweza kuepukwa kwa kulegeza misimamo, kutawaingiza katika baridi ya kisiasa. Umoja wao, ukikitwa kwenye msingi wa msimamo mmoja, unaweza kuwafanya kuamua atakayeunda serikali ijayo kati ya Dkt Ruto na Bw Odinga lakini sio mmoja wao,” asema Kakai.

Vinara wa OKA wanatarajiwa kukutana wikendi kujadili pendekezo la Rais Kenyatta kwamba wamuunge Bw Odinga chini ya mkataba mpya.

Inasemekana kuwa Rais Kenyatta yuko tayari kuwa mdhamini wa mkataba wa kuunda muungano mpya utakaomshinda Dkt Ruto.

Hata hivyo, washirika wa vinara hao wanasisitiza kuwa ni lazima viongozi wa vyama vyao wawe kwenye debe.Kulingana na seneta wa Kitui Enock Wambua, Wiper kilimkabidhi Bw Musyoka tiketi ya kugombea urais pekee.

“Kama chama, mgombea urais wetu ni Bw Kalonzo Musyoka na huo ndio msimamo wake na wa chama,” asema.

Naye mwenzake wa Kakamega Cleophas Malala anasisitiza kwamba vinara wengine wanafaa kumuunga Bw Mudavadi.

“Ninataka kusema wazi kuwa utakuwa kwenye debe. Kuna uvumi kwamba utaunga mtu mwingine kugombea urais. Chama kilikupa tiketi na huo ndio msimamo wetu,” Bw Malala alimwambia Bw Mudavadi.

Kulingana na Bw Kakai, misimamo ya Bw Musyoka na Bw Mudavadi inaweza kuwafanya watorokwe na vinara wenzao katika OKA na kuwatumbukiza katika baridi ya kisiasa.

You can share this post!

Kiongozi wa upinzani nchini Zambia akaribia kuwa Rais

Uhuru, naibu wake wasuka njama ya kuangusha waasi