• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 9:12 AM
JAMVI: Namna Raila anapanga kuyumbisha akina OKA

JAMVI: Namna Raila anapanga kuyumbisha akina OKA

Na BENSON MATHEKA

KIONGOZI wa chama cha ODM Raila Odinga ameweka mikakati tosha ya kuyumbisha muungano wa One Kenya Alliance (OKA) unaoshirikisha waliokuwa washirika wake katika muungano wa National Super Alliance (NASA) ili kuhakikisha hawataungwa mkono na Rais Uhuru Kenyatta walivyotarajia.

Mikakati yake inaonekana kuzaa matunda huku kukiwa na kila ishara kwamba huenda muungano huo ukatibuka.

Wadadisi wa siasa za humu nchini wanasema kwamba moja ya mikakati yake ni kuwagawanya vinara waliomtenga kusuka muungano huo ili kuunyima sura ya kitaifa.

Muungano huo ulileta pamoja vyama vya Wiper cha Stephen Kalonzo Musyoka, Amani National Congress (ANC) cha Musalia Mudavadi, Ford Kenya cha Moses Wetangula na Gideon Moi wa Kanu.

Bw Musyoka, Bw Mudavadi na Bw Wetangula ambao walikuwa washirika wa Bw Odinga katika NASA wamekuwa wakisisitiza kuwa hawatamuunga mkono waziri mkuu huyo wa zamani kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

Akihisi kuwa kutengwa na watatu hao kungemnyima baadhi ya kura alizopata kwenye uchaguzi mkuu wa 2017 na akielewa kwamba wanaweza kushawishika kujiunga na mpinzani wake mkuu, Dkt William Ruto, Bw Odinga aliamua kuyumbisha OKA hata kabla muungano huo kuzinduliwa rasmi.

Kulingana na wadadisi, Bw Odinga alianza kwa kuhakikisha Rais Kenyatta hataunga muungano huo kwa kutumia wandani wake kudai kwamba kulikuwa na watu serikalini waliokuwa wakipanga siasa za urithi bila kumshirikisha.

Madai haya yalitolewa na kiranja wa wachache katika seneti Junet Mohamed aliyedai kwamba baadhi ya maafisa wakuu serikalini walikuwa wameteka mchakato wa Mpango wa Maridhiano (BBI) kwa lengo la kumtenga Bw Odinga.

Madai hayo yalijiri wakati wa chaguzi ndogo za Matungu, Kabuchai na Machakos ambapo Musyoka, Mudavadi, Moi na Wetangula waliungana dhidi ya ODM na kutangaza kwamba watakuwa pamoja kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

“Kwa ODM kudai kwamba watu wenye ushawishi walikuwa wamepanga siasa za urithi wakimtenga kiongozi wao na kwamba walikuwa wameteka mchakato wa BBI ilikuwa njama ya kuvuruga muungano wa OKA. Kumbuka wakati huo, Rais Kenyatta alimtembelea Odinga aliyekuwa akiungua na wakajitokeza pamoja kukagua miradi ya maendeleo,” asema mdadasi wa siasa Geff Kamwanah.

Hii ilifuatiwa na misururu ya mikutano kati ya Bw Odinga na Bw Moi, hatua iliyozua madai ya usaliti katika OKA.

“Moi alitajwa kuwa fuko wa Bw Odinga katika OKA jambo ambalo huenda lina ukweli kufuatia tangazo lake kwamba Kanu haitavunja muungano wake na Jubilee kujiunga na OKA. Kumbuka pia ODM kinasuka muungano na Jubilee. Kuna mkono wa Odinga kwa Kanu kukataa kujiunga na OKA,” asema mdadisi wa siasa Peter Wafula.

Duru zinasema kuwa baada ya juhudi za kushawishi Mudavadi, Musyoka na Wetangula kumuunga Bw Odinga kugonga mwamba, Rais Kenyatta alimshauri Bw Moi kujitenga na OKA na kuungana na Bw Odinga ishara kwamba ameamua kumuunga waziri mkuu huyo wa zamani.

Inasemekana kuwa Bw Odinga amekumbatia wapinzani wa vinara wa OKA katika ngome zao katika juhudi za kuwakata miguu kama njia moja ya kutibua muungano huo.

“Kujiondoa kwa ODM katika muungano wa NASA ni miongoni mwa mikakati ya Bw Odinga ya kuwaonyesha washirika wake kwamba anaweza kupata marafiki wapya wa kisiasa. Kwa mfano, amekumbatia Gavana wa Machakos Alfred Mutua ambaye ni hasimu wa kisiasa wa Bw Musyoka eneo la Ukambani. Hana wasiwasi eneo la Magharibi wanakotoka Mudavadi na Wetangula ambako amekuwa akipata kura kwa wingi na anataka kumkweza Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya,” asema Wafula.

Chama cha Maendeleo Chap Chap cha Dkt Mutua kilimuunga Rais Kenyatta kwenye uchaguzi mkuu wa 2022 sawa na Kanu ingawa hakina mkataba wa ushirikiana na chama tawala cha Jubilee.

Kulingana na Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, chama hicho kimeamua kutafuta washirika wapya kinapojiandaa kwa uchaguzi mkuu wa 2022.

“Tunataka kutafuta marafiki wapya kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022. Hatuwezi kujifunga na marafiki wachache wanaotupatia masharti,” alisema Bw Sifuna.

Duru zinasema kwamba licha ya kujiondoa NASA, Bw Odinga amekuwa akizungumza na waliokuwa vinara wenza katika muungano huo binafsi hatua ambayo wadadisi wanasema ni ya kuwagawanya zaidi.

“Kwanza alihakikisha hawatapata baraka za Rais Kenyatta, pili akapanda mbegu ya usaliti na tatu akafanya wagawanyike ili kuhakikisha hawataungana na Dkt Ruto wote pamoja,” asema Wafula.

You can share this post!

JAMVI: Joho atuliza boli uwanja wa siasa ukialika Nassir,...

MAKALA MAALUM: Kenya yaadhimisha miaka 39 ya jaribio hatari...