• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
JAMVI: Oparanya upanga wa kuifyeka mizizi ya OKA Magharibi

JAMVI: Oparanya upanga wa kuifyeka mizizi ya OKA Magharibi

Na CHARLES WASONGA

MASWALI mengi yameibuliwa kuhusu sababu ya kushirikishwa kwa Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya katika mikutano ambayo Rais Uhuru Kenyatta amekuwa akifanya na viongozi wa upinzani katika Ikulu za Nairobi na Mombasa.

Kwanza, wadadisi wamehoji nafasi ya gavana huyo katika mikutano hiyo ikizingatiwa kuwa yeye si kiongozi wa chama walivyo washiriki wengine kama vile Raila Odinga (ODM), Musalia Mudavadi (ANC), Moses Wetang’ula (Ford-Kenya) na Gideon Moi (KANU).

Pili, japo ikulu imeshikilia kuwa Rais Kenyatta, huitisha mikutano hiyo kujadili athari za janga la Covid-19, mikakati ya kufufua uchumi na masuala yanayohusiana na amani, umoja na uwiano wa kitaifa, duru zasema ajenda kuu huwa ni siasa za urithi wa urais.

Inasemekana kuwa katika mkutano wa Agosti 18, uliofanywa katika Ikulu ya Mombasa, Bw Musyoka alihoji uwepo wa Bw Oparanya katika kikao hicho “ilhali amewakilishwa kikamilifu na Raila.”

“Ni kweli kwamba Kalonzo juzi aliuliza ni kwa nini Oparanya amekuwa akihudhuria mikutano hiyo ilhali chama chake kinawakilishwa na kiongozi wake, Raila Odinga. Lakini majibu aliyopata ni kwamba Gavana Oparanya ni sehemu ya uwakilishi wa ODM katika mikutano hiyo inayoitishwa na Rais,” mmoja wa wandani wa Bw Odinga, ambaye aliomba tulibane jina lake, anasema.

Kwa upande wake, Bw Oparanya juzi alitetea uwepo wake katika mikutano ya Ikulu akisema yeye hupata mwaliko wa moja kwa moja kutoka kwa Rais Kenyatta.

“Kulingana na itifaki, watu wote ambao huenda Ikulu, hufanya hivyo kwa mwaliko wa rais mwenyewe kupitia afisi ya msimamizi wa asasi hiyo. Wale wote wenye maswali yoyote kuhusu wageni wa rais wanapaswa kuyawasilisha kwa asasi husika,” akanukuliwa akisema.

Kwa upande wake mbunge wa Ugunja Opiyo Wandayi ambaye ni Mkurugenzi wa Masuala ya Kisiasa katika ODM, Bw Oparanya hualikwa katika mikutano kati ya Rais Kenyatta na viongozi wa upinzani kwa “sababu ni mmoja wa washirika wa rais katika juhudi zake za kuleta umoja nchini.”

“Ifahamike kwamba Oparanya ni naibu kiongozi wa chama chetu cha ODM. Bw Oparanya amehudumu kwa mihula miwili kama mwenyekiti wa Baraza la Magavana Nchini (COG) sawa na wadhifa wake kama Gavana wa Kakamega. Hii ni kando na kwamba ni yeye pamoja na Waziri Eugene Wamalwa walioteuliwa kushirikisha ajenda ya maendeleo katika eneo la Magharibi ya Kenya,” asema mbunge huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Uhasibu wa Pesa za Umma (PAC).

Mchanganuzi

Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Herman Manyora anakubaliana na Bw Wandayi kuhusu hadhi ya Bw Oparanya, katika eneo la Magharibi na kitaifa.

Lakini kwa mujibu wa msomi huyo ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi, uwepo wa Bw Oparanya katika mikutano hiyo ya Ikulu unalenga “kuyeyusha ushawishi wa Bw Wetang’ula na Mudavadi ndani na nje ya vikao hivyo.”

“Raila huandamana na Oparanya katika mikutano hiyo kwa idhini ya Rais, kuwapa Mudavadi na Wetang’ula ujumbe kwamba endapo watakataa kuunga mkono kiongozi huyo wa ODM katika kinyang’anyiro cha urais mwaka 2022 basi atakwezwa kujaza mapengo yao,” Bw Manyora anasema.

Inasemekana kuwa lengo kuu la Rais Kenyatta ni kuwashawishi vinara wa muungano wa OKA wamuunge mkono Bw Odinga kwa imani kuwa yeye ndiye anaweza kumwangusha Naibu Rais William Ruto debeni.

Lakini Mbw Musyoka na Mudavadi bado wanahisi kuwa kila mmoja wao ndiye anatosha kupambana na Dkt Ruto katika uchaguzi huo.

Naye Bw Wetang’ula ameonyesha ishara kwamba yu tayari kuunga mkono azma ya Bw Mudavadi huku Seneta Gideon Moi akionekana kuwa tayari kuweka kando ndoto yake ya urais na kufuata ushauri wa Rais Kenyatta.

“Binafsi nimewahi kuwashauri ndugu zangu Mudavadi na Wetang’ula kwamba endapo watadiriki kusimama kivyao, bila shaka watafeli. Sasa ni wazi kwamba Rais Kenyatta amejitolea kuunganisha viongozi wote wa upinzani kwa lengo la kumzuia Dkt Ruto kumrithi,” Bw Manyora anaeleza.

Juzi, Rais Kenyatta alionyesha ishara ya wazi wazi kwamba hatamuunga mkono naibu wake katika kinyang’anyiro cha urais 2022, alipomsuta kwa kile alichodai ni mwenendo wake wa kuikosoa serikali.

Katika mahojiano na wahariri wa vyombo vya habari vya humu nchini katika Ikulu ya Nairobi, kiongozi wa taifa alimtaka Dkt Ruto ajiuzulu badala ya kuendelea “kukosoa serikali ambaye yeye bado ni mshirika”.

Bw Javas Bigambo pia anaafikiana na kauli ya Bw Manyora kwamba, Bw Odinga anamkuza Bw Oparanya kwa nia ya kuwadhibiti Mbw Mudavadi na Wetang’ula katika eneo la Magharibi.

“Hii ni kwa sababu wawili hao wameonyesha wazi kwamba hawako tayari kumuunga mkono tena baada ya kuwasaliti katika uliokuwa muungano wa NASA. Sasa Raila ameamua kumtumia gavana Oparanya kama nguzo yake mbadala katika eneo la Magharibi. Hii ndiyo maana Rais humshirikisha katika msururu wa mikutano ya Ikulu,” akasema.

Mapema mwaka huu 2021 Bw Oparanya ambaye ni Naibu Kiongozi wa ODM, alitangaza kuwa atajitosa katika kinyang’anyiro cha urais 2022, lakini hivi sasa anaonekana kuunga mkono azma ya Bw Odinga kutwaa wadhifa huo.

Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho pia alikuwa ametangaza kuwa atawania tiketi ya ODM ili kufanikisha ndoto yake ya kuingia Ikulu.

Hata hivyo, baadaye wawili hawa wameonekana kukunja mkia baada ya Bw Odinga kuimarisha nia yake kuwania urais kwa mara ya tano.

You can share this post!

JAMVI: Ruto kukabiliwa na mtihani mkali 2022 bila ya...

Gent anayochezea Okumu yabebesha mabingwa Club Brugge kapu...