WANDERI KAMAU Na JUSTUS OCHIENG
RAIS William Ruto leo Jumanne anatarajiwa kuongoza mkutano utakaoamua hatima ya mazungumzo baina ya serikali na Upinzani huku Naibu Rais Rigathi Gachagua akibuni mikakati ya kupangua uwezekano wa Kiongozi wa Nchi ‘kukaribisha’ kinara wa Azimio la Umoja Raila Odinga katika serikali yake.
Bw Gachagua ni miongoni mwa vigogo wa Kenya Kwanza ambao wametangaza kutumia kila mbinu kuhakikisha kuwa Bw Odinga anafungiwa nje ya serikali.
Naibu Rais tayari amefanikiwa ‘kunasa’ baadhi ya wabunge, mawaziri na wakuu katika serikali ya Kenya Kwanza ambao wamejitokeza kupinga vikali handisheki. Waziri wa Biashara Moses Kuria na Kiongozi wa Wengi katika Bunge Kimani Ichung’wa ni kati ya majenerali wakuu wa Bw Gachagua wanaoeneza injili ya kupinga handisheki. Alipokuwa akihutubu katika kanisa la AIPCA Limuru, Kiambu, Alhamisi iliyopita, Bw Gachagua alisisitiza kuwa atajitenga iwapo Rais Ruto atakubali ‘kuingiza’ Bw Odinga serikalini.
“Mnaweza kukubali kutazama tu nikijichanganya kupitia handisheki kama Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta?” akauliza Bw Gachagua, akisisitiza kuwa “hawezi kamwe kurudia ‘kosa’ kama hilo”.
Ijumaa ijayo, Bw Gachagua anatarajiwa kuongoza mkutano mkubwa utakaowashirikisha viongozi wa serikali ya kitaifa, idara ya usalama na wengine kutoka kaunti za Murang’a, Kiambu, Nyeri, Nyandarua na Kirinyaga, ambapo inatarajiwa atautumia kuendesha pingamizi zake dhidi ya handisheki. Wadadisi wanasema sababu kuu ya Bw Gachagua kupinga mwafaka huo ni kuhofia kuwa huenda akatengwa kisiasa Rais Ruto akiamua kufanya kazi na Bw Odinga.
Bw Gachagua ameunda kundi la wanasiasa kutoka eneo la Mlima Kenya, ambao wamekuwa wakijitokeza hadharani kukashifu uwezekano wowote wa handisheki baina ya Rais Ruto na Bw Odinga. Kundi hilo linamjumuisha Kiongozi wa Wengi Bw Ichung’wa, maseneta John Methu (Nyandarua), Karungo Thang’wa (Kiambu), Wahome Wamatinga (Nyeri), Gavana Mutahi Kahiga (Nyeri), wabunge Ndindi Nyoro (Kiharu), Faith Gitau (Nyandarua) kati ya wengine. Ijapokuwa wabunge wengi wa mrengo wa Kenya Kwanza wamejitokeza kupinga handisheki, wanasiasa hao ndio wamekuwa wakiongoza juhudi hizo, hasa katika maeneo wanakotoka.
Bw Ichung’wa amekuwa akitumia majukwaa tofauti -kama mikutano ya hadhara na mitandao ya kijamii- kusisitiza kuwa hakutakuwa na handisheki baina ya Rais Ruto na Bw Odinga. Mbinu ya pili ambayo ameibua ni kuhojiwa na vituo vya redio na televisheni vinavyotangaza kwa lugha za Gikuyu, Kimeru na Kiembu, hasa katika eneo la Kati na Mlima Kenya kwa jumla. Mara kadhaa ambayo Bw Gachagua amehojiwa na vituo hivyo, amekuwa akiwaonya wenyeji kuhusu “athari za kiuchumi za handisheki zilizojitokeza Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta alipoamua kushirikiana na Bw Odinga”.
“Handisheki hiyo (ya Uhuru na Raila) ndiyo chanzo cha matatizo yote ya kiuchumi mnayopitia kwa sasa kwani iliharibu kila ajenda yote ya kiuchumi ya serikali ya Jubilee,” akadai Bw Gachagua majuzi. Wadadisi wanasema kuwa kwa kutumia vituo hivyo, lengo lake ni kuwafikia watu wengi zaidi. Bw Gachagua ameanza kutumia mbinu ya kukosanisha Rais Ruto na Bw Odinga, kwa mujibu wa wadadisi.
“Ikiwa Bw Odinga angependa kufanya mazungumzo yoyote na Rais Ruto, lazima kwanza amtambue kama Rais wa Kenya. Ni vipi unaweza kufanya mazungumzo na mtu ambaye hatambui uhalali wako kama rais?” akauliza Bw Gachagua alipohutubu Jumapili katika Kaunti ya Nyeri.
Bw Gachagua alisema kuwa hakuna lolote wanaloweza kuzungumza na Bw Odinga kabla ya kumtambua Dkt Ruto kwani hata kulingana na Katiba, Bw Odinga “ni raia wa kawaida.”
Lakini Bw Javas Bigambo, mdadisi wa masuala ya kisiasa, anasema sharti hilo la Bw Gachagua kumtaka Bw Odinga kumtambua Dkt Ruto kama Rais halali aliyechaguliwa na Wakenya, ni ujanja wa kutaka kuzua uhasama baina ya wawili hao.
Rais Ruto anatarajiwa kutangaza kikosi cha wabunge saba watakaofanya mazungumzo na wenzao wa Azimio katika juhudi za kushughulikia malalamishi ya Upinzani yaliyosababisha Bw Odinga kuongoza maandamano.
Wanaopendekezwa kuketi katika meza ya mazungumzo kuwakilisha upande wa Kenya Kwanza ni Mwakilishi wa Wanawake wa Uasin Gishu Gladys Shollei, Bw Ichung’wah, Kiongozi wa Seneti Aaron Cheruiyot, Kiranja wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Silvanus Osoro, Seneta Maalumu Veronica Maina, mbunge wa Tharaka George Murugara, naibu Kiranja wa Wengi Owen Baya, Kiranja wa Wengi katika Seneti Boni Khalwale, Seneta wa Samburu Steve Lelegwe na Bi Naomi Jillo (Marsabit).
Wanaowakilisha Bw Odinga katika meza ya mazungumzo ni Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Kiranja wa Wachache katika Seneti Ledama Ole Kina, Kiongozi wa Wachache katika Seneti Enoch Wambua na wabunge Otiende Amollo (Rarieda), David Pkosing (Pokot Kusini), Millie Odhiambo (Suba Kaskazini) na Amina Mnyanzi (Malindi).
Duru katika Kenya Kwanza ziliambia Taifa Leo kuwa Bw Gachagua analenga kutumia wandani wake katika kikosi hicho kutatiza shinikizo za kutaka kuwepo kwa handisheki.
Subscribe our newsletter to stay updated