MRENGO wa Kenya Kwanza umejipata lawamani kwa kugeuza hafla zote za maombi ambazo viongozi wake wamekuwa wakihudhuria kuwa jukwaa la kumzungumzia na kumponda kiongozi wa Azimio la Umoja, Raila Odinga.
Ingawa viongozi hao wamekuwa wakishikilia lengo kuu la hafla hizo ni kumshukuru Mungu kwa baraka nyingi alizoijalia Kenya, kinaya ni kuwa hotuba na mahubiri ambayo yamekuwa yakigeuzwa kuwa matamshi ya kumrejelea na kumkashifu Bw Odinga.
Tangu Rais William Ruto na Naibu Rais Rigathi Gachagua kuapishwa kuiongoza nchi Septemba mwaka uliopita, mrengo huo umefanya zaidi ya mikutano kumi ya maombi katika maeneo tofauti nchini.
Hali hiyo ilidhihirika Jumamosi, kwenye hafla ya shukrani iliyojumuisha zaidi ya makanisa 40 katika Shule ya Msingi ya Silungai, eneobunge la Malava, Kaunti ya Kakamega.
Ijapokuwa lengo kuu la hafla hiyo lilikuwa kutoa michango ya kuyasaidia makanisa hayo, viongozi wa kisiasa waliozungumza waliigeuza kuwa ukumbi wa kumshambulia Bw Odinga na washirika wake kwa maandamano ambayo amekuwa akiongoza kila Jumatatu na Alhamisi dhidi ya serikali.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na vigogo wa kisiasa akiwemo Naibu Rais Bw Gachagua, Kiongozi wa Mawaziri Musalia Mudavadi, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, Viongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa na Seneti -Kimani Ichung’wah na Aaron Cheruitot mtawalia, magavana, maseneta, wabunge, madiwani kati ya viongozi wengine. Bw Ichung’wa ndiye aliyeanza kumshambulia Bw Odinga, akimtaja kuwa kiongozi anayefurahia vurugu, maafa na uharibifu wa mali.
“Huyu (Raila) ni kiongozi ambaye furaha yake ni kuona mali ya wananchi ikiharibiwa. Anafaa kukomesha uchochezi huu dhidi ya wafuasi wake. Rais na Naibu Rais ni wazuri kwani wamemvumilia. Ikiwa ni mimi ningekuwa mamlakani, ningekuwa nishamweka gerezani. Nikirudi Nairobi nitamchuna masikio,” akasema Bw Ichung’wa.
Bw Cheruiyot alifuata mkondo uo huo, akimtaja Raila kuwa kiongozi asiyetosheka. “Njia yake ya kupata uongozi ni ghasia. Hajui lugha nyingine. Inasikitisha sana,” akasema Bw Cheruiyot.
Kiongozi huyo alisema kuwa maandamano hayo yatafifia hivi karibuni, kwani Wakenya wamechoshwa na “miito yake ya ghasia”.
Kwa upande wake, Bw Wetang’ula alimrai Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta kumwambia Bw Odinga kukomesha maandamano hayo kwani yeye ndiye rais mstaafu pekee aliyobaki nchini.
“Bw Kenyatta, mwambie ndugu yako (Raila) kukomesha vitendo anavyoendeleza dhidi ya raia kupitia maandamano,” akasema.
Bw Mudavadi alimwambia Bw Odinga kuwa “ujanja wake hatimaye umegunduliwa na jamii ya kimataifa, ndipo imemyamazia hadi sasa.”
Bw Gachagua ndiye aliyefunga ukurasa wa kumshambulia Bw Odinga, akimtaja kuwa kiongozi mwenye uchu wa mamlaka ambaye huwa hatosheki hata kidogo kila matokeo ya uchaguzi mkuu yanapotangazwa.
“Alimsumbua Rais Mstaafu (marehemu) Daniel Moi 1997 ambapo aliingia katika serikali kupitia mlango wa nyuma. Mnamo 2007, alimsumbua Mwai Kibaki, na kufanikiwa kuingia katika serikali yake kama Waziri Mkuu. Mnamo 2017, alifuata mkondo uo huo kwa kumtisha Bw Kenyatta na kufanikiwa kuingia serikalini kupitia handisheki. Mara hii hatafanikiwa. Hatutakubali hata kidogo,” akasema Bw Gachagua.
Pia, Rais Ruto amekuwa akimwelekezea lawama Bw Odinga kupitia hafla za maombi ambazo wamekuwa wakihudhuria. Ikizingatiwa viongozi wa Kenya Kwanza wamekuwa wakishikilia kuwa msingi wa serikali yao ni maombi, wadadisi wanawalaumu kwa “kuzigeuza hafla ya maombi kama jukwaa la kuendeleza siasa”.
“Tungekuwa tukiona kauli hizi zikizingatiwa kikamilifu ikiwa viongozi wangekuwa wakizingatia uhalisia wa kauli zao. Kinaya ni kuwa, vitendo vyao vimekuwa vikikinzana na ahadi zao,” asema mdadisi wa siasa Kipkorir Mutai.
Hata hivyo, mdadisi huyo anawakosoa viongozi wa kidini kwa kuwaruhusu wanasiasa hao kutumia majukwaa ya maombi kujitapa na kuendeleza ukosoaji dhidi ya wenzao. “Viongozi wa kidini pia wanafaa kuelekezewa lawama kwani ndio wamekuwa wakiwaruhusu wanasiasa hao kutumia majukwaa hayo kuendeleza siasa badala ya maombi. Ni mwelekeo hatari unaohatarisha nafasi ya kanisa katika masuala ya kitaifa,” akaeleza mnamo Jumamosi kwenye mahojiano na ‘Taifa Jumapili.’