• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
LEONARD ONYANGO: Siasa zimesaidia wafisadi kuendelea kuponda raha

LEONARD ONYANGO: Siasa zimesaidia wafisadi kuendelea kuponda raha

Na LEONARD ONYANGO

MARA baada ya kutangaza kushirikiana na kinara wa ODM Raila Odinga mnamo Machi 2018, almaarufu handisheki, Rais Uhuru Kenyatta alianzisha operesheni kali dhidi ya wafisadi.

Kila siku Wakenya walishuhudia ‘sinema’ katika runinga maafisa wa idara mbalimbali za mashirika ya serikali wakinaswa na polisi na baadaye kufikishwa kortini chini ya ulinzi mkali.

Baadhi ya wanasiasa na maafisa wakuu serikalini walienda kukamatwa na msururu wa magari ya kifahari.Gangaganga hizo za serikali ziliacha Wakenya na matumaini kwamba mamilioni ya fedha zao zinazoibwa kila siku kupitia ufisadi zingenusurika na badala yake zitumiwe katika miradi ya maendeleo inayofaidi wote.

Japo Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) inasema kuwa imefanikiwa kurejesha zaidi ya Sh20 bilioni kutoka kwa wafisadi tangu 2018, vita dhidi ya ufisadi humu nchini vilimefeli kwa kiwango kikubwa.

Kwa mfano, kati ya 2018 na 2019, EACC inadai ilifanikiwa kubaini mali ya Sh27 bilioni iliyopatikana kwa njia ya wizi wa fedha za umma; lakini tume hiyo ilifanikiwa kurejesha Sh4.5 bilioni pekee.

Kulingana na ripoti ya Hali ya Uchumi ya 2021 iliyoandaliwa na Shirika la Takwimu nchini (KNBS) na kuzinduliwa wiki iliyopita, EACC imemkabidhi Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) zaidi ya faili 500 zinazohusiana na ufisadi tangu 2018.

Lakini hakuna mshukiwa hata mmoja wa ngazi ya juu serikalini ay mwanasiasa ambaye ametupwa gerezani.

Lawama

Badala yake, Rais Kenyatta amekuwa akirushia Idara ya Mahakama lawama kwa kujikokota kusikiliza na kuwahukumu washukiwa.

Kwa upande mwingine, Idara ya Mahakama pia inalaumu DPP kwa kuwasilisha kesi dhaifu bila ushahidi wa kutosha hivyo kuomba kusikilizwa kwazo kuahirishwe mara kwa mara.

Ukweli ni kwamba siasa ndicho kizingiti kikuu ambacho kimezuia Rais Kenyatta kukabiliana na ufisadi ambao wakati mmoja alidai kuwa unasababisha Wakenya kupoteza Sh2 bilioni kwa siku.

Vita dhidi ya ufisadi viliingizwa siasa hivyo imekuwa vigumu kuwanasa wanasiasa pamoja na maafisa wa ngazi za juu serikalini wanaoiba fedha za umma.

Kwa mfano, Gavana wa Kirinyaga Bi Anne Wauguru ambaye alifika Alhamisi mbele ya EACC kujibu maswali kuhusiana na madai ya ufisadi, alidai kuwa aliandamwa kwa sababu alitangaza mpango wa kutaka kugura chama cha Jubilee chake Rais Kenyatta.

Bi Waiguru amekuwa amekuwa akihojiwa na EACC kwa miaka mingi lakini hajawahi kufunguliwa mashtaka kortini.Mbunge wa Mathira Bw Rigathi Gachagua ambaye amekuwa akihojiwa mara kwa mara na EACC, anadai kuwa analengwa kutokana na msimamo wake wa kuunga mkono Naibu wa Rais William Ruto.

Dkt Ruto pia amenukuliwa mara kadhaa akidai kuwa wanandani wake wanasingiziwa mashtaka ya ufisadi kama njia mojawapo ya kutatiza safari yake ya kutaka kumrithi Rais Kenyatta 2022.

Ni wazi kwamba Rais Kenyatta amelemewa na vita dhidi ya ufisadi na hana budi kusalimu amri.

You can share this post!

Pete ya ukeni kinga ya maambukizi ya HIV, wasema watafiti

WANTO WARUI: Wanafunzi walio katika shule za maeneo hatari...