RAIS William Ruto na kinara wa Azimio la Umoja-One Kenya, Bw Raila Odinga wamelegeza misimamo yao na kukubali kufanya mazungumzo.
Bw Odinga alifutilia mbali maandamano yaliyofaa kuendelea leo huku akitoa masharti matano anayotaka yazingatiwe na serikali kabla ya kuanza kwa mchakato wa mazungumzo.
Rais Ruto alikuwa wa kwanza Jumapili kumsihi Bw Odinga kusitisha maandamano ambayo yamekuwa yakifanyika kila Jumatatu na Alhamisi ili kupisha mazungumzo.
Kwa wiki mbili zilizopita, Bw Odinga amekuwa akiongoza wafuasi wake kuandamana huku serikali ikitumia polisi kuwatawanya hatua iliyosababisha vifo na mali kuharibiwa ikiwemo kuchomwa kwa kanisa na msikiti.
Bw Odinga amekataa kutambua ushindi wa Rais Ruto na serikali yake na aliitisha maandamano kushinikiza sava za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) zifunguliwe akidai alipokonywa ushindi, kupunguzwa kwa gharama ya maisha na kusitishwa kwa mchakato wa kuajiri makamishna wapya wa IEBC.
Jana Jumapili, Rais Ruto alisema maandamano hayo yanapaka tope sifa za nchi huku wahuni wakiyatumia kuharibu na kuiba mali.
“Katika wiki mbili zilizopita, watu wamekufa, kujeruhiwa, mali kuibwa au kuharibiwa, uchumi umeathiriwa vibaya na heshima yetu kama nchi imetiwa doa,” alisema kiongozi wa nchi.
Rais Ruto alisema ingawa polisi wamefanya kila wawezalo kulinda maisha na mali ya raia, ghasia zimeendelea kuvuruga mageuzi ya uchumi ya serikali yake. Akisema kuwa uchaguzi wa mwaka jana ulikuwa huru na wa haki, Rais alisema amesikiza malalamishi ya Bw Odinga na yuko tayari wayajadili kwa misingi ya kisheria.
“Nimesikiliza masuala anayozua rafiki yangu, Mheshimiwa Raila Odinga. Katika hali kama ilivyo, sio kuhusu aliye sahihi na asiye sahihi,” alisema Rais Ruto.
Akaongeza: “ Nimekuwa tayari kujadiliana na Wakenya wa matabaka yote, wakiwemo viongozi waliochaguliwa na kuteuliwa kutoka mirengo yote ya kisiasa na viongozi wa kidini kuhusu jinsi ya kufanya nchi yetu kuwa bora na yenye ustawi. Milango yangu ingali wazi kwa mazungumzo ya wazi, nia njema kwa misingi ya sheria na katiba,” alisema.
Na alilegeza msimamo kuhusu mchakato wa kuajiri makamishna wapya wa IEBC ambao Bw Odinga amekuwa akitaka usitishwe akisema unaweza kushughulikiwa na Bunge kwa njia isiyoegemea upande wowote.
“Kwa kuzingatia masuala ambayo yamezuliwa kuhusu hili, ninapendekeza mazungumzo ya pande zote katika Bunge kuhusu kuundwa upya kwa jopo la kuajiri makamishna wa IEBC ndani ya misingi ya kisheria na katiba,” alisema.
Bw Odinga amekuwa akimlaumu Rais Ruto kwa kulenga kuiba uchaguzi wa 2027 kwa kuteua makamishna wa IEBC peke yake, madai ambayo kiongozi wa nchi amekanusha.
Alisema amependekezea Bunge kuunda Afisi ya kiongozi rasmi wa upinzani miongoni mwa mageuzi mengine ambayo yanasubiri kujadiliwa, na suala ya kuajiri makamishna wa IEBC linaweza kujumuishwa katika mdahalo huo. Bw Odinga, hata hivyo, anataka kamati ya Bunge ya kujadili mageuzi ndani ya IEBC, iwe na wenyeviti wawili; kutoka upande wa Azimio na Kenya Kwanza.
Kinara wa Upinzani pia anataka wataalamu wa kimataifa wajumuishwe katika kamati hiyo.
“Kamati hiyo ya Bunge iundwe mara moja na kuanza mazungumzo,” akasema Bw Odinga.
Suala ambalo huenda likazua mvutano katika kamati hiyo, hata hivyo, ni takwa la Bw Odinga kutaka makamishna wanne wa IEBC waliojiuzulu kutokana na shinikizo za serikali warejeshwe kazini.
Bw Odinga pia anataka serikali iachilie huru wafuasi wa Azimio waliokamatwa wakati wa maandamano. Bw Odinga alisema kuwa Azimio wataendelea na maandamano iwapo hakutakuwa na chochote cha maana kitakuwa kimejadiliwa baada ya wiki moja. Upinzani pia unataka serikali kutambua kuwa maandamano ni haki ya kikatiba ya kila Mkenya hivyo wafuasi wa Azimio hawafai kuchokozwa na polisi watakapoandaa maandamano katika siku za usoni.
“Tunataka mashirika ya kijamii yajitokeze kushutumu hatua ya maafisa wa polisi kutumia nguvu kupita kiasi dhidi ya wafuasi wetu wakati wa maandamano,” akasema Bw Odinga.