• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Miraa: Raila aahidi kutafutia wakuzaji soko akiingia ikulu

Miraa: Raila aahidi kutafutia wakuzaji soko akiingia ikulu

Na MARY WANGARI

KIONGOZI wa Orange Democratic Movement (ODM) Raila Odinga ameahidi kutafutia wakulima wa miraa soko katika nchi za kigeni iwapo atachaguliwa kama rais 2022.

Waziri mkuu huyo wa zamani alisema haya Jumatatu katika Kaunti ya Meru wakati wa ziara yake ya siku tatu katika eneo la Mashariki mwa Mlima Kenya, huku Rais Uhuru Kenyatta naye akizuru Kaunti ya Kirinyaga katika maandalizi ya Sherehe za Sikukuu ya Mashujaa itakayoadhimishwa hapo kesho Jumatano.

Rais wa Malawi Lazarus Chakwera akiandamana na mkewe Bi Monica Chakwera ni miongoni mwa wageni mashuhuri wanaotarajiwa kuhudhuria sherehe za Sikukuu ya Mashujaa, kulingana na taarifa kutoka Ikulu iliyofikia Taifa Leo.

“Rais Lazarus Chakwera, akiandamana na mkewe Monica Chakwera, Mama Taifa wa Malawi, atakuwa Mgeni Mheshimiwa katika sherehe za mwaka huu za Sikukuu ya Mashujaa zitakazoandaliwa katika Uwanja wa Wang’uru, Kaunti ya Kirinyaga mnamo Jumatano, Oktoba 20, 2021,” taarifa ilisema.

Iliongeza, “Mnamo Alhamisi, Oktoba 21, 2021, Rais Chakwera na wajumbe wake watapokewa rasmi katika Ikulu, Nairobi na wenyeji wake Rais Uhuru Kenyatta na Mama Taifa Margaret Kenyatta.”

Sherehe hizo zinatarajiwa Kirinyaga huku juhudi za kuwapatanisha viongozi mahasimu kutoka eneo hilo zikishika kasi kabla ya hafla hiyo ya kitaifa.

Wakenya wanasubiri Sikukuu hiyo kwa hamu huku wengi wao wakitumai kwamba serikali hatimaye itafutilia mbali kafyu ya kitaifa iliyotangazwa katika juhudi za kukabiliana na Covid-19.

Akijibu wito huo, Kiongozi wa Taifa alidokeza kwamba serikali itaondoa kafyu hiyo hivi karibuni bila kufafanua ni lini hasa.

Mnamo Jumatatu, Rais Kenyatta alikutana na viongozi wa Kaunti ya Kirinyaga, wakiongozwa na Gavana Anne Waiguru, katika Sagana State Lodge, Kaunti ya Nyeri.

Rais Kenyatta aliwahimiza viongozi hao kuungana na kufanya kazi pamoja ili kufanikisha maendeleo ya haraka katika kaunti hiyo.

Aidha, alitahadharisha dhidi ya siasa za uongo na maneno matupu akisisitiza kuwa njia pekee ya kuwezesha ustawi ni kupitia amani na utangamano unaopatikana kupitia uongozi mwema.

Alitaja mradi wa Bwawa la Thiba unaogharimu Sh8.5 bilioni kama mojawapo ya miradi mikuu inayotekelezwa na serikali na inayotazamiwa kubadilisha uchumi wa kaunti hiyo na taifa kwa jumla.

“Tumetekeleza miradi hii kwa sababu ya ushirikiano na amani miongoni mwa viongozi ambao umehakikisha kwamba hatubadilishi tu maisha ya wakazi wa Kirinyaga ila pia raia wote wa Kenya. Wakulima wetu wa mpunga sasa wanapata bei bora kwa mazao yao. Kupitia Bwawa la Thiba tutaweza kupanua kilimo cha mpunga ili kukidhi mahitaji ya humu nchini. Tunafaa kukuza na kula kitokacho humu nchini mwetu,” alisema Rais Kenyatta.

Kuhusu zao la miraa, Kiongozi wa ODM aliapa kusuluhisha mzozo mkali kuhusu mpaka kati ya Kenya na Somalia ili kuhakikisha zao la miraa linaendelea kuuzwa katika taifa hilo la Afrika.

Aliahidi pia kutafutia zao hilo ambalo ni maarufu katika Kaunti ya Meru, soko katika mataifa ya kigeni ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ikiwa juhudi zake za kumrithi Rais Kenyatta 2022, zitafua dafu.

“Ninajua wakulima wa miraa wamepata shida kubwa kwa kukosa soko. Soko letu la Somalia linadidimia, mara wamefunga mara wamefungua… Nitahakikisha ya kwamba Somalia inafungua mipaka yake na miraa inaenda huko. Kuna sehemu ya Somalia ambayo imekuwa huru, inaitwa Somaliland, tayari wamekubali kuchukua miraa kwetu, lakini Somalia imezuia ndege zetu kupita na kupeleka miraa huko. Tutatatua shida hiyo, ndege zetu zitoke hapa hadi zifike Somalia,” alieleza.

You can share this post!

Bodi yasaka chanzo cha jengo kuporomoka

DPP ataka kesi za Kimwarer, Arror ziunganishwe

T L