NA MWANDISHI WETU
NAIBU Mwenyekiti wa chama kikubwa cha United Democratic Alliance ndani ya mrengo tawala wa Kenya Kwanza, Seth Panyako amejiuzulu kutoka kwa wadhifa huo akisema anapinga mpango wa serikali kutoza wafanyakazi asilimia tatu ya mishahara ili kujenga nyumba za bei nafuu.
Bw Panyako ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Muungano wa Kitaifa wa Wauguzi (KNUN) ametangaza Jumamosi akiwa kwenye mazishi ya mwanasiasa Joseph Hamisi katika Kaunti ya Kakamega.
“Nilizungumza na Rais William Ruto na kilichobainika wazi ni kwamba siwezi nikaendelea kuwa Naibu Mwenyekiti wa UDA wakati ninapinga mpango huo wa wafanyakazi kutozwa asilimia tatu ya mishahara kufanikisha ujenzi wa nyumba,” amesema Bw Panyako.
Kwa mujibu wa Bw Panyako, sera za uchumi katika serikali inayoongozwa na Ruto zitawafukuza wawekezaji na kuwarudisha nyuma waajiri pamoja na wafanyakazi.