GEORGE ODIWUOR Na BENSON MATHEKA
RAIS William Ruto anaendelea na mikakati ya kijanja yenye lengo la kupenya ngome za kinara wa Azimio la Umoja, Raila Odinga, hasa Nyanza huku akihimiza miungano ya Kenya Kwanza na Azimio kufanya mazungumzo ya maridhiano bungeni.
Kati ya mbinu za kisiasa ambazo Dkt Ruto anatumia ni kuwashawishi wabunge kadhaa kutoka ngome za Bw Odinga wahamie upande wa serikali, kuteua walioshindwa uchaguzini katika serikali yake na kuwatumia kutoa ahadi na kutekeleza miradi ya maendeleo.
Rais Ruto amekuwa akitembelea eneo hilo na pia kutuma washirika wake kujaribu kushawishi wapigakura kumuunga mkono mapema kuelekea 2027 huku akinuia kuvunja kinachotajwa kama laana ya Nyanza kutounga mgombea urais mwingine isipokuwa Bw Raila.
Dkt Ruto anatumia mbinu ambazo wadadisi wanasema inasubiriwa kuona iwapo zitabadilisha akili za wakazi wa ngome ya Raila kumuunga mkono Nyanza. Bw Odinga aliye na ufuasi mkubwa eneo hilo anashikilia kuwa alishinda urais na anashinikiza sava za Tume ya Uchaguzi (IEBC) zifunguliwe hata mazungumzo yaliyoitishwa na Rais Ruto.
Huku akihimiza pawepo mazungumzo hayo ili kuepuka maandamano yaliyosababisha vifo na uharibifu wa mali, Kiongozi wa Nchi amerushia minofu kaunti za eneo la Nyanza ‘vinono’ na kutuma washirika wake kusimamia miradi mashinani ili wakazi wahisi serikali inawajali. Tayari, washirika wake wamefungua ofisi kadhaa za chama chake cha UDA katika kaunti za Kisumu na Siaya.
Mipango ya kufungua ofisi ya chama hicho katika kaunti ya Homa Bay imekamilika. Washirika wa Ruto katika eneo hilo wanaojumuisha aliyekuwa gavana wa Nairobi, Dkt Evans Kidero, aliyekuwa gavana wa Kisumu Jack Ranguma, mwenzao wa Migori Okoth Obado na wabunge Gideon Ochanda (Bondo), Elisha Odhiambo (Gem), Mark Nyamita (Uriri), Caroli Omondi (Suba South), Shakeel Shabir (Kisumu East, Huru), Paul Abuor (Rongo), John Owino (Awendo) na seneta wa Kisumu Tom Ojienda wamekuwa wakihubiri “injili ya maendeleo”.
Bw Nyamita amekuwa akiwataka wakazi wa Nyanza kuunga serikali kwa kuwa Rais Ruto ameanzisha miradi ya maendeleo katika eneo lao.
Maafisa wa UDA wamekuwa wakihusika katika shughuli zinazonuiwa kumuongezea umaarufu Rais Ruto na serikali yake. Kwa wakati huu, maafisa hao wanaendelea kusajili wanachama huku duru zikisema wanalenga watu 250,000 ndani ya miezi mitatu.
Chama hicho kinachoongozwa na Rais Ruto tayari kimepokea wanachama wa Bw Odinga wakiwemo madiwani wa zamani walioshindwa katika uchaguzi wa mwaka 2022.
“Shughuli hizi zote ni ujanja wa kuwavutia wapigakura wamuunge Rais Ruto ambaye hakuna kinachomzuia kugombea urais 2027,” asema mchambuzi wa siasa Derrick Ouma.
Baadhi ya maafisa wakuu wa serikali wamekuwa wakitembelea kaunti za Nyanza huku wakiwarai wakazi kuunga serikali ya Rais Ruto ambayo Bw Odinga anasisitiza hatambui. Rais Ruto pia ameteua baadhi ya viongozi wanaokosoa Bw Odinga katika serikali yake.
Miongoni mwao ni Waziri wa Habari, Mawasiliano (ICT) na Uchumi wa Dijitali Eliud Owalo, na Dkt Kidero ambaye ni waziri msaidizi.
Hata hivyo, Bw Ouma anasema kwamba itakuwa mlima kwa Dkt Ruto kutikisa umaarufu wa Bw Odinga katika eneo la Nyanza.
“Sidhani itakuwa rahisi kununua wakazi wa eneo la Ziwa kwa miradi ya maendeleo ambayo wanaamini ni haki yao. Hata hivyo, kuna juhudi za UDA kutumia ujanja kupenya eneo hilo huku serikali ikiteka Bw Odinga na wito wa mazungumzo,” asema.
Bw Odinga amelaumu Kenya Kwanza kwa kununua wabunge wa upinzani.