NA BENSON MATHEKA
MAKATAA ya wiki moja ambayo kiongozi wa Azimio la Umoja Raila Odinga alimpa Rais William Ruto kufanikisha maridhiano, au vinginevyo, muungano huo wa Upinzani urudie maandamano, yanamalizika leo Jumatatu, huku upande wa serikali ukiwa umepiga hatua chache.
Katika tamko linaloweza kuwa kizingiti kwa mchakato wa maridhiano, Naibu Rais Rigathi Gachagua jana Jumapili alitoa takwa kwa Bw Odinga akimtaka atambue Dkt Ruto kama rais kwanza.
“Kabla ya sisi kukubali kuzungumza naye (Odinga), ni lazima atambue hadharani kwamba Rais William Ruto ni rais wa Kenya. Suala la kuzungumza hata halipo kwa sababu anasema hamtambui William Ruto kama Rais. Kwa hivyo, unawezaje kuzungumza na mtu ambaye hatambui uhalali wako,” akasema Bw Gachagua akiwa katika kanisa la PCEA, Ngorano, Nyeri.
Aprili 2, Bw Odinga alikubali ombi la Rais Ruto la kusitisha maandamano ili kutoa nafasi kwa harakati ya mazungumzo kupitia bunge kuhusiana na takwa la upinzani la kuajiri makamishna wapya wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
“Tunakubali mchakato wenye usawa wa bunge unaosimamiwa na pande zote mbili na unaosaidiwa na wataaalamu kutoka nje . Kama hakutakuwa na mazungumzo ya maana kutoka kwa Ruto (Rais) maandamano yataanza tena katika muda wa wiki moja,” Bw Odinga alisema alipotangaza kusitisha maandamano.
Alhamisi, Azimio iliteua kamati itakayowakilisha mrengo wake kwenye meza ya mazungumzo huku makataa ya Bw Odinga kwa serikali kuonyesha kujitolea kwake kwa maridhiano yakikamilika leo Jumatatu.
Kamati hiyo inajumuisha Maseneta Ledama ole Kina (Narok), Edwin Sifuna (Nairobi), Enoch Wambua (Kitui), na wabunge David Pkosing (Pokot Kusini), Otiende Amollo (Rarieda), Millie Odhiambo (Suba Kaskazini) na Amina Mnyanzi (Malindi).
Huku Bw Gachagua akitoa sharti jipya kwa Bw Odinga, mrengo wa Kenya Kwanza bado haujakutana kuteua wabunge watakaouwakilisha katika mazungumzo. Wabunge wa Kenya Kwanza wanatarajiwa kukutana Jumanne ijayo kuteua wawakilishi wake.
Wiki jana Rais Ruto alikutana na viongozi wa muungano tawala wa Kenya Kwanza bungeni ambapo inasemekana aliwaagiza kufanikisha mchakato wa mazungumzo huku Bw Odinga akikutana na wabunge wa Azimio na kuteua wawakilishi watakaoongoza mazungumzo.
Hata hivyo, takwa la Azimio la kusisitiza kuwa ni lazima sava za IEBC zifunguliwe kubaini mshindi wa uchaguzi wa urais kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka jana limekataliwa na upande wa Serikali.
Katika ombi lake kwa upinzani kusitisha maandamano, Dkt Ruto alisema uchaguzi mkuu ulikuwa wa haki na suala hilo lilikuwa limeamuliwa na Mahakama ya Upeo lakini kuundwa kwa IEBC kunaweza kujadiliwa kupitia mchakato wa bunge.
Hata hivyo, kwenye mkutano na wanahabari baada ya kushauriana na vinara wenza katika Azimio, Bw Odinga alitilia shaka mchakato wa bungeni na kutaka mazungumzo yafanywe nje ya bunge na kuhusisha wadau wengine.
“Pendekezo letu ni kuwa na mazungumzo katika kiwango cha kitaifa kupitia mchakato unaofanana na Muafaka wa Kitaifa wa 2008. Muungano wetu unapendekeza kikosi kiundwe kutoka bungeni na nje ya Bunge,” Bw Odinga alisema.
Pendekezo lake lilikataliwa na upande wa serikali uliosisitiza lazima mazungumzo yoyote yafanyike katika bunge huku kiongozi huyo wa ODM akisisitiza Azimio itarudia maandamano upande wa serikali ukionyesha dalili za “kuwachezea shere”.
“Tunawahakikishia wafuasi wetu na Wakenya kuwa hatujaacha azima yetu na kusisitiza kuwa tutarudi kwa wananchi kukiwa na dalili za kukesekana kwa umakinifu kutoka kwa upande ule mwingine,” alisema.
Haya yanajiri huku maafisa wastaafu wa kijeshi wakitaka mdahalo wa kitaifa utakaohusisha wadau wengine wakidai bunge linaegemea upande wa serikali na masuala yanayoibuliwa na Upinzani siyo ya kisiasa pekee. Viongozi wa kidini pia wanataka wajumuishwe katika mazungumzo hayo ya maridhiano wakisema yatafanikiwa zaidi yakihusisha watu wote.
“Nchi hii ni yetu na kila mmoja anafaa kuhusishwa. Itakuwa bora watu wote wakijumuishwa,” alisema Katibu Mkuu wa Baraza la Kitaifa la Makanisa Kenya.