• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
Wafalme wa kuhadaa vijana

Wafalme wa kuhadaa vijana

Na LEONARD ONYANGO

WANASIASA sasa wanatumia ahadi hewa kama chambo cha kunasa kura za vijana huku Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9, 2022 ukikaribia.

Naibu Rais William Ruto na kinara wa ODM Raila Odinga ni miongoni mwa wanasiasa wanaomezea mate urais mwaka ujao ambao wamekuwa wakitoa ahadi tele za ‘danganya toto’ kwa vijana.

Kati ya Wakenya milioni 19.6 waliojisajili kuwa wapigakura 2017, vijana wa kati ya umri wa miaka 18 na 35 walikuwa asilimia 51, kulingana na ripoti ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Katika shughuli ya usajili wa wapigakura kwa wingi inayoendelea kote nchini, IEBC inalenga kusajili wapigakura wapya milioni 6, wengi wao wakiwa vijana.

Karibu asilimia 60 ya wapigakura mwaka ujao watakuwa vijana –hali ambayo imefanya wanasiasa kuwang’ang’ania kwa kutoa ahadi ambazo hawatatimiza baada ya kuchaguliwa.

Jumamosi, Bw Odinga alipokutana na vijana mjini Naivasha, Kaunti ya Nakuru, aliahidi kutoa Sh6,000 za bwerere kwa kila kijana asiye na ajira kila mwezi iwapo atachaguliwa kuwa rais.

Shirika la Takwimu nchini (KNBS) linakadiria kwamba kuna watu milioni 2.49 – wengi wao wakiwa vijana – wasiokuwa na ajira.

Hiyo inamaanisha kwamba iwapo Bw Odinga atachaguliwa kuwa rais wa tano wa Kenya, atawapa vijana wasio na ajira Sh180 bilioni za bwerere kila mwaka.

Wataalamu wa masuala ya kiuchumi, hata hivyo, wametilia shaka ahadi hiyo huku wakisema kuwa itakuwa vigumu kuitekeleza.

Bw Odinga pia ameahidi kwamba vijana watakaoanzisha biashara hawatalipa ushuru kwa miaka saba kuwezesha biashara zao kukua.

Ameahidi kuongeza kiasi cha mikopo ya elimu ya juu (Helb) kwa kuzingatia gharama ya maisha na vijana wanaokamilisha masomo yao hawataingizwa kwenye orodha ya watu wanaoshindwa kulipa mikopo (CRB).

Iwapo Bw Odinga atashinda urais, zaidi ya vijana 1,000 wanaohitimu masomo yao, watakuwa wakipokea mishahara huku wakifanya mafunzo ya nyanjani katika mashirika ya kimataifa, ikiwemo Umoja wa Mataifa (UN).

Kinara wa ODM pia ameahidi kuunda wizara huru ya Vijana na kubuni hazina maalum ya wahudumu wa bodaboda.

“Nitabuni hazina spesheli ya kusaidia wahudumu wa bodaboda. Kiwanda cha kuunda pikipiki kitakuwa humu nchini. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kwamba zaidi ya vijana milioni 2.4 wanapata pikipiki kwa bei nafuu,” akasema Bw Odinga.

Kwa sasa vijana wako chini ya wizara ya Habari na Teknolojia ya Mawasiliano (ICT), Ubunifu na Masuala ya Vijana.?Dkt Ruto jana, huku akiwa ziarani katika Kaunti ya Isiolo, aliendelea kumimina ahadi zake kwa vijana.

“Chama cha UDA (United Democratic Alliance) ndicho kinachojali masilahi ya wananchi wa kawaida. Tutawapa vijana nafasi za ajira, mikopo nafuu na mazingira bora ya kuanzisha biashara,” akasema Dkt Ruto baada ya kuhudhuria ibada katika Kanisa Katoliki la Isiolo.

Bw Odinga, kiongozi wa Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi na Spika wa Bunge Justin Muturi –ambao wote wametangaza kuwania urais mwaka ujao – wameelezea kutoridhishwa na idadi ndogo ya vijana wanaojitokeza kujisajili kuwa wapigakura.

Wadadisi wanasema kuwa hali hiyo inasababishwa na hatua ya wanasiasa kutoa ahadi hewa kila baada ya miaka mitano.?Serikali ya Jubilee, kwa mfano, haijatekeleza kiasi kikubwa cha ahadi ambazo Rais Uhuru Kenyatta na Dkt Ruto walitoa 2013 na 2017.

Miongoni mwa ahadi walizotoa kwa vijana ni kubuni nafasi za ajira milioni 1.3 kila mwaka. Lakini ahadi hiyo haijatimizwa.

“Ahadi yetu kwa vijana ni kuhakikisha kuwa wanapata ujuzi unaohitajika kujiletea mapato humu nchini na ngazi ya kimataifa, kuwasamehe kulipa ushuru na kuwapa mikopo nafuu,” inasema manifesto za Jubilee 2013 2017.

Ahadi nyingine ambazo Rais Kenyatta na Dkt Ruto walitoa 2013 lakini hazijatimia ni kujenga vituo vya ICT na maktaba katika kaunti zote 47, viwanja vya michezo vitano katika kila kaunti, kujenga viwanja vya michezo vya kitaifa Kisumu, Mombasa, Nakuru, Eldoret na Garissa.

Wawili hao pia waliahidi kujenga Taasisi za Teknolojia katika kila wadi ili kuwezesha vijana kujiinua, mafunzo ya bila malipo katika vyuo vya ufundi, kutenga asilimia 2.5 ya mapato ya nchi kwa ajili ya Hazina ya Ustawishaji Vijana (YEF).

You can share this post!

Wetang’ula apuuza Eseli mzozo ukitokota Ford- Kenya

Mipasuko UDA na Jubilee yaibua vyama vipya Mlimani