• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
‘Tiktoker’ Azziad Nasenya apuuzilia mbali uvumi kwamba ‘kuna mubaba nyuma ya ufanisi wake’

‘Tiktoker’ Azziad Nasenya apuuzilia mbali uvumi kwamba ‘kuna mubaba nyuma ya ufanisi wake’

NA FRIDAH OKACHI

‘TIKTOKER’ maarufu nyumbani na ughaibuni, Azziad Nasenya, amesema alipata kazi katika Wizara ya Michezo kutokana na bidii na kisomo chake, huku akiwataja wanaodai kuwa anatumia hongo za ngono kama watu wasiojielewa.

Mwanahabari huyo mwenye umri wa miaka 23, kwenye mahojiano na Mungai Eve mnamo Novemba 13, 2023, alifafanua vigezo vya yeye kupata kazi ya masuala ya vijana, michezo na sanaa kwenye wizara hiyo.

Bi Nasenya alisema alipewa kazi kutokana na sifa zake bila kuwa na uhusiano wowote wa kimapenzi.

Alishangaa jinsi wanaomfuatilia kwenye mitandao ya kijamii walivyomshambulia na kudai hawezi kupata nafasi hiyo kwa jasho na bidii yake isipokuwa vinginevyo.

“Ukiangalia, mimi nimeenda shule, akili ninayo. Singekuwa hapa nilipofikia iwapo sina akili,” alisema Bi Nasenya.

 “Nimeenda shule, nimemaliza. Mimi ni mwanafunzi katika Taasisi ya Mawasiliano ya Umma ya Kenya. Taaluma yangu ya uanahabari ndiyo ninafanya kazi katika redio. Unamaanisha nini kwamba sistahili? Unamaanisha nini?” alimjibu Bi Mungai.

Mwanahabari huyo alisema shutuma za aina hiyo humfanya ahisi vibaya. Vilevile alifahamisha mwenye kipindi kuwa ana mpenzi anayemsaidia kukabiliana na masuala kama hayo. Alitaja wazazi wake kuwa kiungo muhimu katika ukuaji na umaarufu wake.

“Nina mpenzi ambaye namshukuru sana kwa kuniunga mkono. Yeye na wazazi wangu ni watu ambao hunipigia simu kujua ninaendelea vipi,” alieleza.

Mnamo Agosti 25, 2023, Waziri wa Michezo Ababu Namwamba alikanusha madai ya kuwepo kwa huba baina ya wawili hao, akitaja uvumi huo kuwa unyanyasaji wa mtandaoni na kumwonea huruma mwanadada huyo.

Bw Namwamba alijitetea na kusema wakati mwingine wanaoshikilia nafasi kwenye afisi za serikali, kuna baadhi yao ambao huendeleza porojo za aina hiyo ili kuwachafulia majina.

Mapema mwaka 2023, wawili hao walikisiwa kuwa wapenzi baada ya wawii hao, kila mmoja, tena kivyake, kuchapisha picha kwenye mitandao ya kijamii, lakini kwa sadfa wakawa wamevalia viatu vilivyokuwa vinafanana.

‘Tiktoker’ huyo alichapisha picha akiwa Dubai kwa mapumziko ya siku kadhaa akiwa amevalia viatu aina ya Converse rubber sawa na waziri huyo aliyechapisha picha akiwa amevalia jozi ya viatu aina hiyo.

  • Tags

You can share this post!

Mwago sasa adai baadhi ya machifu Starehe ni...

Maji ya mafuriko yatatiza usafiri katika barabara kuu ya...

T L