• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 12:48 PM
KIPUTE CHA TIM WANYONYI: Leads United inapigiwa chapuo kufanya ukweli

KIPUTE CHA TIM WANYONYI: Leads United inapigiwa chapuo kufanya ukweli

Na JOHN KIMWERE

TIMU ya Leads United inapigiwa chapuo kuzamisha Ngamia One FC na kusonga mbele kwenye mechi za kuwania taji la Tim Wanyonyi Super Cup 2021 katika uga wa UoN CAVS, Nairobi.

Nao wachana nyavu wa Kibagare Slums wamepangwa kuchuana na Wazoefu FC huku Potters ikigarazana na Buffalo FC uwanjani humo. Wazoefu FC itashiriki mchezo baada ya kuangusha Lopez FC kwa mabao 5-0. Leads United ya kocha, Wilston Issa inapigiwa upatu kuendeleza ubabe wake kwenye kampeni hizo baada ya kunyamazisha Kibagare Sportiff kwa bao 1-0 kwenye mechi ya kwanza.

”Katika mpango mzima tunataka tujikaze kiume tuhakikishe tunashinda mechi zote na kutwaa tiketi ya fainali ya mwaka huu ambapo tumepania kuhifadhi kombe hilo,” kocha huyo wa Leads alisema. Leads United ambayo hushiriki Ligi ya Taifa Daraja la Pili inajivunia huduma za sajili wapya wanaotazamiwa kuchochea wenzao kwenye michezo hiyo.

Timu inategemea wachana shupavu kama Kelvin Juma, Herman Ngala, Benito Kambele, Bernard Odhiambo, Michael Onyango na Calvin Odhiambo kati ya wengine. Kwenye ratiba ya mechi hizo katika uga wa Kihumbu-ini, Kangemi Nairobi, Kangemi Atletico imepangwa kumenyana na CAVS nayo Simba FC itaumana na Kabete Technical FC huku wachezaji wa Dreams FC wakipepetana na Kitusuru Allstars.

Picha/JOHN KIMWERE

Kangemi Atletico ilinasa tiketi ya kushiriki patashika hiyo iliposajili ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Gachie Youth. Mashindano ya mwaka huu ambayo ni makala ya nane yalivutia jumla ya timu 64 za wanaume na 14 za wanawake. Leads United na Kibagare Girls ndio mabingwa watetezi kitengo cha wanaume na wanawake mtawalia. Leads ilibeba taji hilo ilipogaragaza Leverkusen FC mabao 4-2 kupitia mipigo ya matuta baada ya kutoka bao 1-1.

Picha/JOHN KIMWERE

You can share this post!

Joho ashinikiza sera za mizigo bandarini zibadilishwe

Ukikutana na hizi ‘kanda mbili’ utajua ni za...

T L