• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
Mukidza kuwa nahodha wa Kenya Simbas ikipepetana na Wahispania Barcelona Alhamisi

Mukidza kuwa nahodha wa Kenya Simbas ikipepetana na Wahispania Barcelona Alhamisi

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA Darwin Mukidza atakuwa nahodha wa Kenya Simbas itakapomenyana na Wahispania Diables Barcelona katika mechi ya mwisho kwenye ziara ya Afrika Kusini mnamo Novemba 25.

Vijana wa kocha Paul Odera wamekuwa na kipindi kimoja cha mazoezi ugani Toyota mjini Bloemfontein hapo Jumatano.Mukidza amesema kuwa wako tayari kwa kibarua dhidi ya Barcelona.

“Motisha iko sawa kikosini na wachezaji kadhaa wana hamu kubwa kwa sababu watakuwa wakicheza kwa mara ya kwanza katika ziara hii na wengine watapata fursa ya kucheza kwa mara ya pili. Pia, wamepata kushika kasi katika mazoezi yetu na kuona Diables Barcelona wanavyocheza raga.

Naamini tuko tayari kwa mchuano huo na ninahakikishia mashabiki wetu kuwa tutajitolea kadri ya uwezo wetu tutakapojibwaga uwanjani hapo kesho (Novemba 25),” alisema Mukidza.Mkurugenzi wa Raga, Thomas Odundo aliongeza kuwa baada ya kuwa na mechi tatu ngumu, waliona itakuwa busara kupumzisha wachezaji ambao wamecheza dakika nyingi.

“Tulisafiri na kikosi cha wachezaji 33 na tungependa kuwatumia wote katika ziara hii… Tunahisi kuwa tumepata mazoezi mazuri sana katika ziara hii,” aliongeza Odundo.

Simbas, ambayo ilipoteza dhidi ya Carling Champions 87-15 (Novemba 6) na Namibia 60-24 (Novemba 14) na kubwaga Brazil 36-30 (Novemba 20), itapepetana na Barcelona saa kumi na mbili unusu jioni mnamo Alhamisi. Mechi hiyo itapeperushwa kwenye runinga ya Super Sport Channel 211.

Kikosi cha Simbas dhidi ya Diables Barcelona:

Wachezaji 15 wa kwanza – 1. Joseph Odero, 2. Bonface Ochieng, 3. Patrick Ouko, 4. Brian Juma, 5. Thomas Okeyo, 6. George Nyambua (naibu wa nahodha), 7. Fidel Oloo, 8. Stephen Sakari, 9. Barry Robinson, 10. Darwin Mukidza (nahodha), 11. Derrick Ashihundu, 12. John Okoth, 13. Peter Kilonzo, 14. Andrew Matoka, 15. Isaac Njoroge. Wachezaji wa akiba – 16. Ian Njenga, 17. Eugene Sifuna, 18. Ephraim Oduor, 19. Bethwel Anami, 20. Elkeans Musonye, 21. Brian Wahinya, 22. Vincent Onyala, 23. Jacob Ojee, 24. Daniel Sikuta, 25. Malcolm Onsando, 26. Jone Kubu.

You can share this post!

Wanasoka walemavu kutoka Kenya kuenda Tanzania kushiriki...

Twaha Mbarak kuwania urais FKF

T L