• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 PM
Dereva chipukizi Yuvraj alenga changamoto mpya kwenye Autocross kwa kupanda daraja

Dereva chipukizi Yuvraj alenga changamoto mpya kwenye Autocross kwa kupanda daraja

Na GEOFFREY ANENE

YUVRAJ Rajput yuko tayari kwa changamoto mpya baada ya kubeba taji la kitaifa la kitengo cha Bambino kwenye Mbio za Magari na Vigari maarufu kama Autocross wakati wa raundi ya tisa kwenye bustani ya Twisty Corners katika kaunti ya Kiambu.

Yuvraj, ambaye ni mtoto wa dereva wa mbio za magari Kirit Rajput, alihifadhi ubingwa wa kitaifa baada ya kumzidia ujanja mpinzani wake wa karibu Karamveer Rooprai mnamo Jumapili.

Alirejesha kigari chake cha Magi-Bug cha injini ya 500cc katika nafasi ya pili akiwa na muda wake bora kwenye mizunguko minne wa dakika 6:56.37. Amaan Ganatra alitwaa taji la duru hiyo ya tisa kwa dakika 5:47.07 naye Rooprai akaridhika na nafasi ya tatu (6:59.83).

Baada ya kuhifadhi taji mnamo Jumapili, Yuvraj maarufu kama Yuvi ametangaza kuwa atapanda daraja kushiriki kitengo cha chipukizi cha 2WD Non-Turbo, ambacho vigari vinavyoshiriki vina nguvu zaidi.

“Nafurahi sana kushinda msimu kwa mara ya pili mfululizo. Barabara za duru hii ya tisa zilikuwa na udongo tifutifu, lakini za kusisimua kwa mashindano. Mwaka ujao, naingia kitengo cha chipukizi cha 2WD Non-Turbo ninachotarajia kiwe na ushindani mkali kutoka kwa Neel Gohil na Brandon Ng’ang’a,” alisema Yuvraj aliyetawala kitengo cha Bambino mwaka 2019 kabla ya mashindano ya 2020 kufutiliwa mbali baada ya mkurupuko wa virusi vya corona.

Gurraj Singh alinyakua ubingwa wa kitengo cha Quad baada ya bingwa mtetezi Wayne Fernandes kukamata nambari mbili katika Twisty Corners.

Gurraj alikamilisha kwa dakika 3:02.40 dhidi ya Fernandes (4:38.53).

Kiana Rajput alitawala kitengo cha Pee Wee kwa kumzidia maarifa Eann Bengi. Mwanadada huyo aliandikisha 9:55.34 naye Eann hakumaliza mizunguko ya tatu na nne.

Kiana ananusia kutawazwa malkia wa Pee Wee msimu huu. Anahitaji tu kushiriki duru ya mwisho ili kutimiza sharti la asilimia 75 ya mashindano. Duru ya mwisho ya Autocross ni Desemba katika eneo ambalo bado halijatangazwa.

You can share this post!

Miguna Miguna adai serikali imemzuia kurejea nchini

Jinsi ya kuandaa biriani ya nyama ya n’gombe

T L