• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 8:50 AM
Badi aapa kuwakabili wanaotatiza kazi jijini

Badi aapa kuwakabili wanaotatiza kazi jijini

Na WANDERI KAMAU

MKURUGENZI Mkuu wa Idara ya Huduma za Jili la Nairobi (NMS), Meja Jenerali Mohamed Badi, amesema anafahamu mwenyewe jinsi atayakabili makundi ya watu wenye ushawishi ambayo yamekuwa yakiingilia utendakazi katika jili la Nairobi.

Jenerali Badi aliwataja watu hao kuwa “Wakenya wa kawaida”, akisema hawatamtatiza kwa vyovyote kutoa huduma muhimu kwa wakazi wa Nairobi.

Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni Jumatano usiku, Jenerali Badi alitoa mfano wa jinsi makundi hayo yalijaribu kumzuia kutimiza malengo yake kwa kuchoma kituo cha kutengeneza lami lakini yakashindwa.

“Watu hao ni Wakenya wala si raia wa kigeni, hivyo tunafahamu jinsi ya kukabiliana nao. Walijaribu kunizuia kutimiza malengo yangu kwa kuchoma kiwanda cha kutengeneza lami, japo walinichelewesha kwa wiki tatu pekee. Niliepuka mtego wao,” akasema.

Kulingana naye, kuna makundi ya watu wenye nia ya kuendelea kufaidika kwa usimamizi mbaya wa jiji kuu.

Gavana Mike Sonko amekuwa akilalamikia “mwingilio” wa makundi hayo kwenye utendakazi wake, akiyataja “kuteka” karibu idara zote muhimu za serikali yake.

Mwaka uliopita, alimrai Rais Uhuru Kenyatta kumsaidia kuliendesha jiji, akisema makundi hayo yalikuwa yakitishia uongozi wa serikali yake.

“Nakuomba Rais utusaidie kuyakabili makundi hayo kwa kuchukua baadhi ya majukumu ya kaunti ili kuyazuia kutuingilia,” akasema Bw Sonko.

Jumatano, Jenerali Badi alirejelea mikakati ya halmashauri hiyo kulistawisha jiji, akisema lengo lake kuu ni kuendesha mikakati ya maendeleo kwa kumshirikisha kila mmoja.

Alisema miongoni mwa wale ambao amefanikiwa kushirikisha kwenye mikakati hiyo ni familia zinazoishi barabarani na mitaani, maarufu kama “chokoraa.”

“Cha kushangaza ni kuwa tumeshirikiana na baadhi ya familia hizo kuyasafisha baadhi ya maeneo jijini,” akaeleza.

Hata hivyo, alilalamikia hatua ya Bw Sonko kukataa kuidhinisha bajeti ya kaunti kama changamoto kuu inayomkabili katika kutimiza baadhi ya mipango ya halmashauri hiyo.

“Tuna mipango mingi tuliyo nayo lakini hatua ya Gavana Sonko kutoidhinisha bajeti imeathiri sana baadhi ya mipango yetu, ikiwemo kuwalipa madaktari mishahara,” akaeleza.

Wiki mbili zilizopita, Bw Sonko alikataa kuidhinisha Mswada wa Bajeti ya Kaunti 2020/2021, akisema bajeti hiyo “ilifanyiwa mageuzi” bila taratibu zifaazo kuzingatiwa. Kaunti ilikuwa imetengewa jumla ya Sh37.7 bilioni.

Bunge la Kaunti lilikuwa limepitisha bajeti ya Sh35.5 bilioni, huku NMS ikitengewa Sh27.1 bilioni nazo idara anazoshikilia Sonko zikitengewa Sh6.4 bilioni. Bunge lilitengewa Sh2 bilioni zilizobaki.

Bw Sonko alikataa kuidhinisha mswada huo akilalamikia “kubaguliwa” na Serikali ya Kitaifa.

Bw Sonko na Jenerali Badi wamekuwa wakitofautiana vikali, gavana akidai kuwa lengo kuu la mkurugenzi huyo ni “kutwaa” mamlaka yake.

You can share this post!

Wamuua kaka yao wakipigania mahari ya dada

Miradi ya barabara hatarini Mombasa